Miss Tanzania, Salha Israel azama Bongo Movie

Muktasari:

Mrembo Salha Israel, ambaye alivaa taji la Miss Tanzania mwaka 2011/2012 ameamua rasmi kuingia kwenye tasnia ya uigizaji baada ya msimu wake wa urembo kuisha.


Mrembo Salha Israel, ambaye alivaa taji la Miss Tanzania mwaka 2011/2012 ameamua rasmi kuingia kwenye tasnia ya uigizaji baada ya msimu wake wa urembo kuisha.


Mrembo huyo amefungua milango yake kuelekea kwenye kazi ya kuigiza filamu za kitanzania kupitia kampuni ya RJ Company katika kazi yake ya kwanza inayoitwa “Bud Luck”, Salha Israel ataonyesha uwezo wake pamoja na wakali wengine kwenye bongomovie kama Batuli na Johari.


Salha ameiambia Mwananchi kwamba amechagua uigizaji kuwa kazi yake mpya kwa sasa, na kwamba mashabiki wategemee mengi kutoka kwake


Akiongeza kwenye mazungumzo hayo Miss Tanzania huyo ambaye alimaliza kutumikia taji lake vizuri bila kupata skendo zozote mbaya alisema,”Kufanya movie ilikuwa ni moja ya ndoto zangu kubwa. Nilikuwa na mawazo kwamba hata ningeshindwa kupata taji la Miss Tanzania basi ningeingia moja kwa moja kwenye uigizaji. Lakini ilinibidi nisubili kidogo baada ya kushinda taji lile na muda ndio huu umefika”.


Salha hatakuwa mrembo wa kwanza kuingia kwenye uigizaji kwani Wema Sepetu, Aunty Ezekiel na Irene Uwoya ambao wote ni baadhi ya waigizaji wa kike wanaofanya vizuri hivi sasa kwenye uigizaji, wamepata umaarufu kwanza kupitia mashindano ya urembo Tanzania maarufu kama Miss Tanzania.