Diamond kuingiza sokoni albamu mpya

Muktasari:

  • Albamu hiyo ni ya tatu kwa mwanamuziki huyo, baada ya Kamwambie na Lala Salama.

Dar es Salaam. Mshindi wa tuzo ya mwanamuziki bora wa kiume Afrika Mashariki kwa miaka minne mfululizo katika tuzo za Afrimma, Diamond Platnumz ametangaza ujio wa albamu mpya aliyoipa jina la A Boy From Tandale.

Hii itakuwa albamu ya tatu kwa mwanamuziki huyo, baada ya Kamwambie na Lala Salama.

Taarifa zimeeleza baadhi ya nyimbo zitakazokuwemo kwenye albamu hiyo ni Number One na Number One Rmx, Nasema Nawe, Bum Bum, Nitampata wapi na Nana.

Mwanamuziki huyo anayetamba na wimbo mpya wa Hallelujah, amesema yupo kwenye maandalizi ya mwisho kutengeneza kazi hiyo ambayo ni maalumu kwa mashabiki wanaopenda muziki wake.

Diamond jana Jumatano aliutumia ukurasa wake wa mtandao wa Instagram kuwataarifu mashabiki kuhusu kazi hiyo mpya akiandika, “Album soon come, #ABoyFromTandale”.

Alipoulizwa na MCL Digital, meneja wa mwanamuziki huyo, Salaam Sharaf amesema huo ni ujio mpya wa mwanamuziki huyo ambao utakuwa na mambo mengi ya kushangaza ndani yake. Alipotakiwa kuelezea albamu hiyo itauzwa wapi na itasambazwa vipi, Salaam alijibu: “Tuna mengi ya kuzungumza kuhusu albamu hii na namna itakavyowafikia mashabiki wetu, watu wavute subira tutaliweka wazi jambo hili hivi karibuni.”