Kuchepuka: Sio Diamond tu, hata Kevin Hart, Schwarzenegger, Kris Jenner

Muktasari:

  • Kati ya skendo kubwa za usaliti zilizowahi kuwakumba viongozi miaka ya hivi karibuni ni Bill Clinton akiwa rais wa Marekani na François Hollande akiwa Rais wa Ufaransa. Yalizungumzwa yakaisha lakini yanabaki kwenye historia.

Unakumbuka mkasa wa Bill Clinton na Monica Lewinsky au François Hollande na Julie Gayet.

Kati ya skendo kubwa za usaliti zilizowahi kuwakumba viongozi miaka ya hivi karibuni ni Bill Clinton akiwa rais wa Marekani na François Hollande akiwa Rais wa Ufaransa. Yalizungumzwa yakaisha lakini yanabaki kwenye historia.

Mwanzo wa wiki hii mitandao ya kijamii Tanzania ilipamba moto. Wapenzi wa burudani walioko huko walikuwa wakizungumza mada moja tu …Mtoto wa Hamisa Mobeto na Diamond Platnumz. Hili lilikuwa ikiwa ni baada ya takriban wiki tatu za kuwapo kwa tetesi kwamba, ujauzito alikuwa nao mrembo huyo ni wa Diamond.

Awali, Diamond alikataa katakata tuhuma hizo kiasi kwamba hata aliandika mstari kwenye remix ya wimbo wa Fresh wa Fid Q akithibitisha kwamba kinachozungumzwa na baadhi ya watu ni kusingiziwa tu licha ya kuwepo shahidi mbalimbali za kimazingira zilizokuwa zikimbana ikiwemo mama mzazi wa Diamond kwenda hospitali alipojifungulia Mobeto.

Lakini baada ya mtoto kuzaliwa na kupewa jina la baba mzazi wa Diamond, picha zinazomwonesha Mobeto na Diamond wakiwa kwenye malavidavi zikaanza kusambazwa— huku ikidaiwa kuwa zilisambazwa makusudi kumkomesha kwa kuwa alimkataa mtoto.

Lakini baada ya mambo kuwa magumu Diamond aliamua kwenda kwenye kituo cha redio na kukiri kwamba ni kweli anafahamu kuwa yeye ndiye mtoto wa Mobeto.

Sasa suala hapa halikuwa tu kuhusu Diamond kumkataa mtoto, bali pia kukiri kwa Diamond kuhusu mtoto wa Mobeto ni sawa kabisa na kukiri kwamba alimsaliti mpenzi wake aliyezaa naye watoto wawili na kumvisha pete ya uchumba Zari —jambo ambalo matokeo yake yanasubiriwa kwa hamu hadi hivi sasa.

Hata hivyo, si Diamond pekee aliyewahi kukumbwa na maswahibu haya — wapo mastaa wengine nje ya Tanzania, waliowahi kuchepuka, siri ikavuja, wakakiri kwa namna moja ama nyingine.

Arnold Schwarzenegger

Mwaka 1991, mwigizaji na Gavana Mstaafu wa Jimbo la California, Marekani, Arnold Schwarzenegger pamoja na aliyekuwa mke wake kwa kipindi hicho, Maria Shriver walimwajiri Mildred Baena kama msaidizi wa nyumbani.

Hata hivyo, kumbe nyuma ya mgongo wa mke wake, Schwarzenegger alikuwa akitoka kimapenzi na Baena ambaye naye pia alikuwa ni mke wa mtu kwa kipindi hicho na uhusiano huu wa siri, ulifika mbali zaidi ambapo Baena alibeba ujauzito ambao ilithibitika kuwa ni baada ya miezi tisa, mtoto alipozaliwa, ilithibitika kuwa ni wa damu ya Schwarzenegger.

Kwa sababu hiyo, Baena aliachana na mume wake ambaye alikuwa akidhani kuwa yeye ndiye muhusika wa mimba aliyoibeba mkewe, wakati Arnold naye alikubali kwamba yeye ndiye baba wa mtoto aliyezaliwa na Baena na akapewa jina la Joseph.

Mwaka 2011 baada ya Arnold kumaliza muda wake wa ugavana, alikaririwa na vyombo vya habari akieleza kwamba alimuweka wazi mke wake kuhusu mtoto aliyezaa na Baena, hiyo ikiwa ni miaka zaidi ya miaka, na pia iliripotiwa kwamba kwa kipindi chote hicho Arnold alikuwa akimuhudumia mtoto wake kwa siri jambo ambalo linadaiwa kuwa lilisababisha mke wake kuomba talaka na wakatengana mwaka huo.

Tiger woods

Anatajwa kama ni miongoni mwa wacheza gofu waliopata mafanikio makubwa kimichezo na kiuchumi pia.

Mwaka 2010 Woods alitalakiana na mke wake Elin Nordegren ambaye alizaa naye watoto wawili huku sababu ya kuachana kwao ikithibika waziwazi kwamba ni mchezo mchafu wa kuchepuka alioufanya Woods.

Kilichotokea ni kwamba, mwaka 2009 Elin aligundua kuwa Woods anachepuka na mwanamke aitwaye Rachel Uchitel na kwa mujibu wa simulizi za Elin mwenyewe, anasema arobain za mwizi zilitimia usiku ambao Woods alikuwa nyumbani amelala.

Elin akachukua simu ya mume na kuanza kupekua ambapo alikuta meseji ya mume wake kwenda kwa Rachel ikisema: “Wewe ni mtu wa pekee niliyewahi kumpenda.”

“Nimekumiss.” Elin akatuma meseji nyingine ya namna hiyo akijifanya ni Woods ambapo baada ya muda, Rachel alijibu kwa kuuliza lini wataonana tena.

Tangu hapo hakukuwa na msalie mtume, Elin akamuamsha mume na nyumba ikawaka moto.

Hata hivyo, mwaka 2010, Tigerwoods alikiri kosa mbele ya vyombo vya habari na ndani ya mwaka huo huo walitalakina na Elin.

Kevin Hart

Kevin Hart ni muigizaji wa Marekani ambaye naye ni mmoja wa mastaa waliojaribu kuchepuka lakini kwa bahati mbaya wakanasa na siri zikavuja.

Kwa sasa Kevin ni mume na baba wa watoto wawili wawili aliozaa na mke wake Eniko Parrish ambaye pia ni mjamzito.

Wiki iliyopita, mitandaoni ilisambaa video inayomuonyesha Kevin Hart akiwa mtupu chumbani na mwanamke ambaye si mke wake. Kwa lugha nyepesi, alikuwa akichepuka.

Hata hivyo Hart alijaribu kupinga kile kilichosambaa lakini kwa muda mfupi sana alishindwa kuendelea kusimamia uongo wake na aliamua kukiri na hata kuomba radhi kwa mke wake, watoto, mashabiki na watu wake wa karibu kupitia ukurasa wake katika mtandao wa kijamii wa Instagram.

Brad Pitt

Brad Pitt ni muigizaji wa Marekani ambaye aliwahi kuwa mume wa Angelina Jolie. Lakini kabla ya kuwa na Angelina, Brad Pitt alikuwa ni mume wa muigizaji Jennifer Anniston ambaye walitalakiana mwaka 2005 baada ya Brad kutokuwa muaminifu kati ndoa yake. Brad Pitt alikuwa akichepuka na Angelina na kunogewa mpaka alipofumwa.

Brad alichepuka na Angelina Jolie, ambaye walikutana wakati wanatengeza filamu ya Mr and Mrs Smith ambayo waliigiza kama mume na mke.

Hata hivyo, licha ya kwamba mchepuko wa Brad Pitty ulifanikiwa kuwa mke, kwa sasa hawapo pamoja tena kutokana na kutengana mwishoni mwa mwaka 2016.

David Beckham

Mume wa mke mmoja na baba watoto wanne. Ni mwanasoka mstaafu aliyetamba mwanzoni mwa miaka ya 1990 hadi 2000 alipokuwa akiitumikia timu ya Manchester united.

Mwaka 2003 alisajiliwa na timu ya Real Madrid ya Hispania na alipoanza kazi huko alikutana na mrembo Rebecca Roos ambaye baadae akawa mfanyakazi wake akimtumikia kama msaidizi binafsi.

Baadaye iligundulika kuwa Beckham na Rebeca sio tu walikuwa ni mtu na bosi wake, bali pia walikuwa wanatoka kimapenzi. Baada ya Rebeca kuacha kazi kwa Bechkam mwaka 2004, alifichua siri hiyo katika gazeti la News to The Word… hata hivyo, Beckahm hakuibuka kupinga juu suala hilo wala kukiri jambo ambalo linawafanya watu waunganishe nukta na kupata jibu. Beckham alikuwa na nafasi ya kutumia mahakama ili labda kulipwa fidia ya kuchafuliwa na gazeti lililochapisha habari hiyo.

Kristen Stewart

Supastaa wa filamu za Twilight, Kristen Stewart alikumbwa na skendo ya usaliti baada ya kufumwa na mwongozaji wake wa filamu za Hunts Man, Rupert Sanders.

Kristen aliyekuwa katika uhusiano na mwigizaji mwenzake, Robert Pattinson alijikuta katikati ya dunia ya usaliti baada ya paparazzi kupiga picha akijicinjari ndani ya gari na mwongozaji huyo.

Ni moja kati ya skendo za kukumbukwa kwani Kristern na Pattinson walikuwa wakitajwa kama ‘Power Couple’ wa Hollywood wakilinganishaw na Angelina Jolie na Brad Pitt kwa wakati huo.

Kris Jenner

Mama wa familia ya kina Kardashian, Kris Jenner amewahi kukiri kuchepuka wakati akiwa ameolewa na Robert Kardashian kwamba alifanya mchezo huo akiwa na mwongozaji wa filamu aliyocheza. Jenner alisema: “Ukiwa mdogo unafanya mambo mengi ya kukufadhaisha, ninachojutia ni kuwa nilimsaliti mume wangu.”

Chris Rock

Mchekeshaji maarufu duniani Chris Rock aliachana na mkewe baada ya kukiri kuchepuka na mwanamke mwingine. Ndoa yake na

Megalyn Echikunwoke ilivunjika na sasa ameanzisha uhusino mwingine akijiapiza kuwa mwaminifu.