Muktasari:

Inawezekana pirika zimefanya upitwe na baadhi ya habari kubwa zilizojiri wiki hii. Hii hapa orodha ya habari tano zilizopamba vichwa vya habari

Inawezekana pirika zimefanya upitwe na baadhi ya habari kubwa zilizojiri wiki hii. Hii hapa orodha ya habari tano zilizopamba vichwa vya habari

 Diddy mweusi pekee miongoni mwa matajiri wenye ‘bongo’

Rapa na mfanyabiashara P Diddy alijikuta katika jukwaa moja na matajiri wa dunia katika sherehe za miaka 100  za Jarida la Forbes. Diddy alitajwa kuwa miongoni mwa wafanyabiashara 100 wenye bongo ( Greatest Living Business Minds).

Wafuasi wa Kenyatta washambuliwa na kundi la nyuki

 Wakati jopo la majaji watano wa mahakama kuu nchini Kenya wakisoma sababu za kufuta matokeo ya urais nchini Kenya, waandamanaji wengi wao wakiwa wafuasi wanaomuunga mkono Rais Uhuru Kenyatta walivamiwa na nyuki na kulazimika kujisalimisha ka kuondoka katika eneo hilo.

Nyuki hao walioibuka ghafla walisababisha eneo hilo kufanana na lile liliondolewa na askari kwa nguvu kwani kila mmoja alikimbia kujificha.

 Mamia ya watu wafariki dunia Mexico

Mexico imekumbwa na tetemeko la ardhi ambalo limesababisha vifo vya watu zaidi ya 240 na wengine wengi wakiwa bado wanatafutwa katika vifusi.

Tetemeko hilo linalodaiwa kuwa na ukubwa wa 7.1 limeanguja nyumba zaidi ya 30 katika mji wa Mexico City na watoto 30 hawajulikani walipo.

 Diamond akiri kuchepuka

Jumanne wiki hii mwanamuziki Diamond Platnumz alisimamisha shughuli za watu mbalimbali wote wakitega macho na masikio katika redio na televisheni za Clouds Media Group wakifuatilia ‘akiungama’ kuzaa na mwanamitindo Hamisa Mobetto. Katika mahojiano hayo yaliyodumu wa saa tatu Diamond alimwomba msamaha mpenzi wake Zari ambaye amezaa naye watoto wawili.

 Trump ataka Korea Kaskazini iangamizwe

Majuzi Rais wa Marekani, Donald Trump alihutubia baraza la Umoja wa Mataifa na kusema amechoshwa na tambo za Korea Kaskazini akisema sasa wakati umefika wa kuiangamiza nchi hiyo. Hata hivyo, Trump aliurusha mpira kwa Umoja wa Mataifa akisema imshughulikie kwa kuwa ndio kazi yake.