
| DK Slaa amvaa mke wa Kikwete | Send to a friend |
| Thursday, 02 September 2010 22:50 |
Salim Said, BabatiKAMPENI za uchaguzi mkuu zimezidi kunoga baada ya mgombea urais wa Chadema, Dk Slaa kumgeukia mke wa Rais Jakaya Kikwete akieleza kuwa anatumia vibaya rasilimali za nchi kumpigia kampeni mumewe huku akimtaka katibu mkuu wa CCM, Yusuph Makamba aeleze kisa cha kufukuzwa ualimu mkuu wa shule ya msingi. Kwa muda mrefu Salma Kikwete, mke wa Rais Kikwete na ambaye pia ni mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (Wama), amekuwa katika ziara kwenye mikoa mbalimbali, jambo ambalo limekuwa likitafsiriwa kuwa anafanya ziara za kampeni kwa ajili ya mumewe. Kwa sasa yuko mkoani Manyara. Akizungumza kwenye mkutano wa kampeni, Dk Slaa ambaye ameripotiwa kuwa na makombora 20 kwa ajili ya kuimaliza CCM, alisema kitendo cha mke huyo wa rais kumpigia kampeni kwa kutumia rasilimali za umma ni ufisadi. “Mke wa rais si rais," alisema Dk Slaa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Kwara ulio Babati Mjini. "Mama Salma anatembea na askari wa serikali; magari ya serikali na wakuu wa mikoa na wilaya. Anatumia fedha za Ikulu kwa sababu walinzi wake wanalipwa na Ikulu. Huu ni ufisadi.” Dk Slaa, ambaye alikuwa mbunge wa Karatu kwa tiketi ya Chadema), aliongeza kusema: “Nimepita huko nimeambiwa (mke wa rais) anatembea na msafara wa magari 20 na kila gari moja lina thamani ya Sh200 milioni ambayo pia yanatembea kwa mafuta ya serikali. Ni ufisadi. “Kama mke wa rais anatembea na msafara wa magari 20, je rais mwenyewe atatembea na msafara wa magari mangapi? Wakati mgombea urais wa Chadema akitembea kwa basi, mke wa rais anatembelea magari ya serikali. Ni ufisadi mkubwa kutumia magari hayo kwa maslahi binafsi.” Aliyeanza kumlipua Mama Kikwete katika mkutano huo ni mkurugenzi wa kampeni wa Chadema, Suzan Kiwanga ambaye alidai kuwa kama mke huyo wa rais anataka kushiriki kwenye siasa angesajili chama na kuchukua fomu ya kugombea badala ya kutumia Wama. Kiwanga alidai kuwa Mama Kikwete anafanya ziara hizo bila ya ratiba iliyoidhinishwa na Tume ya Uchaguzi (Nec), akimpigia debe mumuwe jambo ambalo ni kinyume cha sheria. “Nataka nimwambie huyu mtu aitwaye Mama Salma kwamba kiherehere chako kitakufikisha mahali pabaya. Unatumia fedha za wanawake za Wama kwa maslahi yako... ni kinyume cha sheria,” alisema Kiwanga huku akishangiliwa. Makombora ya Dk Slaa hayakuishia kwa Mama Salma pekee, bali pia kwa katibu mkuu wa CCM, ambaye alinukuliwa na vyombo vya habari akisema mgombea urais huyo wa Chadema anateswa na ndoa yake baada ya kuachana na Rose Kamili aliyezaa naye watoto wawili na kuanza uchumba na Josephine Mushumbusi. Dk Slaa, ambaye ametangaza hadharani suala la kuachana na mwanamke ambaye alizaa naye watoto wawili na kuanza uchumba na Josephine, alisema: “Tukisema tuanze kutaja nyumba ndogo za kila mwanasiasa hapa, nani atabaki? Sasa naanza na Makamba. Namtaka anieleze kwa nini alifukuzwa nafasi ya ualimu mkuu katika shule ya msingi?” Dk Slaa hakutaja sababu iliyomfanya Makamba afukuzwe ualimu mkuu wa shule ya msingi, lakini akaahidi kuwa atatoboa siri hiyo iwapo katibu huyo mkuu wa CCM hataueleza umma ukweli. “Nyinyi wananchi hamjui kama Makamba alikuwa mwalimu mkuu wa shule ya msingi... mimi najua sasa anieleze kwa nini alifukuzwa kama mwalimu mkuu? Asiposema mimi nitamaliza,” aliahidi Dk Slaa huku umma ukimsikiliza kwa makini. Makamba, ambaye ni luteni wa zamani wa jeshi, hakupatikana jana kuzungumzia suala hilo. Kuhusu mwandani wake, Dk Slaa alisema: “Ni kweli niliishi na mwanamke na kuzaa naye, lakini sikufunga naye ndoa. Nilipotaka kufunga ndoa nilimtaka huyu. Kwani nani anamchagulia mtu mke.” Taarifa zinaonyesha kuwa Dk Slaa alikuwa anaishi na Rose Kamili ambaye alikuwa diwani wa CCM Karatu. Diwani huyo wa zamani wa CCM sasa amekihama chama hicho na kujiunga na Chadema. Dk Slaa alisema baada ya kukutana na Josephine, walipendana na kuamua kufunga ndoa. “Sasa namuuliza Makamba ni ndoa gani hiyo inamtesa Dk Slaa,” alihoji mgombea huyo urais kwa tiketi ya Chadema ambaye amebobea kwenye sheria. Kuhusu madai ya Makamba kuwa aliasi dini kwa kuamua kuachana na uaskofu, Dk Slaa alisema Chadema haitafuti uaskofu wala ushehe kwa sababu kama wangekuwa wanatafuta uaskofu, angekwishaupata miaka 20 iliyopita. Baada ya hapo, Dk Slaa alimgeukia aliyekuwa mbunge wa Babati Mjini, Omar Kwaangw’ kwamba CCM inasema Dk Slaa ananuka ukatoliki. “Babati ni nyumbani na ndio maana nimeamua kulisemea hili hapa kwa sababu nawapenda watu wa Babati na pia nilipopata upadri mlikuja Karatu kusheherekea,” alisema Dk Slaa. Alisema wakati akiwa padri na mkurugenzi wa Maendeleo ya Jimbo Kuu la Mbulu, alijenga Shule ya Sekondari ya Singe na kumwajiri Omar Kwaangw’ kwenye shule hiyo ya kanisa lakini hakuambiwa kuwa si mkatoliki. "Nilipokuwa mbunge wa Karatu wakasema nitawezaje kuwachunga watu wa Karatu kwa madai kuwa nimeshindwa kuchunga upadri. Je nawauliza watu wa Babati nimeshindwa kuwachungwa watu wa Karatu?” alihoji na kujibiwa: “Hukushindwaa baba.” Alisema aliyoyafanya Karatu hayakuchagua Mkatoliki, Mlutheri wala Mwislamu bali kila mtu alifaidika na ubunge wake baada ya kuishinikiza serikali kushusha kodi ya kichwa nchi nzima na kufuta michango ya Mwenge wa Uhuru wilayani Karatu. “Tukiingia Ikulu ili kulinda heshima ya baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, kwa sababu aliuwasha juu ya Mlima Kilimanjaro ili umuilike Afrika nzima, tutauchukua na kuuhifadhi katika jumba la makumbusho Dar es Salaam ili uwe maonyesho,” alisema Dk Slaa. “Pia tutafuta kodi zote za manyanyaso kwa Watanzania sambamba na kurudisha rasilamali zote za umma chini ya serikali ya Watanzania.” Baada ya hapo, Dk Slaa alimgeukia mgombea ubunge wa Babati Mjini (CCM), Kisyeri Chambiri akimtuhumu kuwa ni fisadi na hafai kuwa mbunge kwa sababu alitimuliwa kazi alipokuwa mkandarasi wa barabara ya Galapo-Kimotorok wilayani Simanjiro. “Dk Slaa hasemi kwa kuropoka bali ana data (ushahidi). Katika jibu la swali namba 103 bungeni linasema 'baada ya kuona mkandarasi wa barabara ya Galapo kupitia kampuni ya Weasons anasuasua amefukuzwa kazi rasmi'. Hivyo mtu akifukuzwa kazi ya umma hafai kuwa mbunge,” alisema Dk Slaa. “Lakini pia Chambiri amepata nafasi ya kugombea ubunge wa Babati kwa rushwa, hivyo hawezi kupiga vita rushwa na atazidisha rushwa katika halmashauri.” Dk Slaa aliongeza kusema: “Chambiri anadai kuwa aliondoka Tarime kwa hiari, muulizeni alikutana wapi na Dk Slaa? Maana Dk Slaa ni miongoni mwa waliomfukuza Chadema mwaka 2005 tulipokwenda kumuona marehemu Chacha Wangwe.” Chacha Wangwe alikuwa mbunge wa Tarime kwa tiketi ya Chadema na alifariki kwa ajali ya gari iliyotokea nje kidogo ya mkoa wa Dodoma wakati akisafiri kwenda Dar es salaam. Dk Slaa alimtaka Waziri wa Fedha, Mustapha Mkullo aeleze ni lini bunge gani lilithibitisha na kupitisha nyongeza ya mishahara ya wafanyakazi wa umma katika bajeti ya serikali ya 2010/11. “Kama makamu mwenyekiti wa kambi ya upinzani bungeni, nimepitia kifungu kwa kifungu katika bajeti yote ya serikali ya 2010/11, sikuona kipengele cha nyongeza ya mishahara, lakini wameongeza mishahara kinyemela baada ya rais kusema hahitaji kura 300,000 za wafanyakazi," alisema Dk Slaa. Alikuwa akizungumzia taarifa za nyongeza ya mishahara ya wafanyakazi wa umma ambazo zilibainika siku chache baada ya Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (Tucta) kutaarifu kuwa lingemtangaza mgombea urais anayeungwa mkono na wafanyakazi. Tucta ilisema kuwa mgombea ambaye angetangazwa ni yule ambaye "anataka pilau lao" baada ya Rais Kikwete kueleza kwenye kikao na wazee wa Dar es salaam kuwa serikali haiwezi kuongeza kima cha chini cha mshahara wa wafanyakazi wa sekta ya umme hadi Sh315,000 na kwamba "kama ni hizo kura za wafanyakazi, basi sizitaki". Dk Slaa aliwataka wananchi wa Babati waachane na ushabiki wa chama na wajadili maisha na maendeleo yao ili kumpata mtu atakayewaongoza vizuri. Dk Slaa aliwanadi wagombea ubunge wa majimbo ya Babati Mjini Pauline Gekul na Babati Vijijini Francis Qamara pamoja na wagombea wa udiwani wa kata za majimbo hayo. Akiwa wilayani Kiteto, Dk Slaa alieleza mikakati yake atakapoingia Ikulu kuwa ni pamoja na kufumua mikataba yote iliyoingiwa kati ya serikali na wawekezaji na kuiunda upya ili imletee faida Mtanzania wa kawaida. Dk Slaa alisema serikali yake itahakikisha rasilimali za Watanzania zinatumika kwa maslahi yao wenyewe na si watu wachache. “Ndugu zangu mkitupa ridhaa yenu, naahidi kwamba tutafumua mikataba yote kati ya serikali na wahisani, ili tuondoe upotevu mkubwa wa fedha unaotokana na mikataba mibovu iliyosainiwa na serikali,” alisema Dk Slaa. Dk Slaa alisema kila mwaka Tanzania inapoteza zaidi ya Sh700 bilioni kutokana na mikataba mibovu iliyoingiwa kati ya serikali na wawekezaji. “Fedha zipo za kutosha kuondoa hali mbaya ya maisha ya watanzania, kinachokosekana ni utashi wa kisiasa wa watanzania, upendo wao na imani yao kwa Chadema,” alisema Dk Slaa na kuongeza: “Inawezekana kabisa ndugu zangu na katika kufanikisha hili hatuhitaji fedha za kigeni. Wenzetu Kenya hivi sasa huduma zote za afya, elimu na jamii ni bure. Wamewezaje hata sisi tushindwe?” alihoji Alisisitiza kuwa, “Wakenya hawana madini sisi tunayo, hawana gesi sisi tunayo, hawana uranium sisi tunayo, tuna mengi kuliko wakenya, kwa nini wao waweze na sisi tushindwe au tumelaaniwa sisi, la bali ni utawala mbovu wa Chama cha Mapinduzi.” |
| Last Updated on Saturday, 04 September 2010 09:02 |



Salim Said, Babati









