Wawili wanaodaiwa wapenzi wauawa kwa kuchomwa moto

Muktasari:

Uchunguzi unaendelea kubaini chanzo cha moto huo.

Arusha . Watu wawili wanaodhaniwa ni wapenzi,  wameuawa kwa kuchomwa moto baada ya kufungwa kamba wakiwa kitandani, katika  tukio lililotokea eneo la Whiterose lililoko kata ya Kiranyi wilayani Arumeru mkoani hapa.

Mamia ya watu wamejitokeza  kuzunguka nyumba lilipotokea tukio hilo baada ya kuona moshi ukitoka katika moja ya chumba na kuonekana miili ikiwa imeteketea kwa moto.
Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha,Charles Mkumbo amesema tuki hilo limetoke leo, Jumanne saa 3.00 asubuhi

Amesema aliyekutwa amefariki ni  Maurine Urio (32)  pamoja na rafiki yake huyo ambaye hajaweza kutambulika kutokana na kuungua sana.

“Tumepata taarifa asubuhi hii kuwa kuna nyumba inaungua na polisi pamoja na zimamoto walifika eneo la tukio na kukuta watu hao wameshapoteza maisha wakiwa juu ya godoro ambako mwanaume alionekana kabla ya kuchomwa alifungwa kamba miguu na mikono ili kuzibitiwa,”amesema.

Mkumbo amesema miili ya marehemu imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya mkoa Mount Meru huku wahusika wa tukio hilo wakiwa wanatafutwa.

Akizungumzia tukio hilo mwenyekiti wa mtaa wa Ilkiurei iliyoko kata ya Kiranyi, Onesphory Chami amedai kuwa tukio hilo linahusishwa na wivu wa mapenzi.