Sophia Simba aandika historia

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania, Sophia Simba akiteta jambo na wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM katika Ukumbi wa White House mjini Dodoma kabla ya kikao cha NEC kuanza ambacho kilipitisha maamuzi ya kumfuta uanachama wa chama hicho mwishoni mwa wiki. Picha ya maktaba

Muktasari:

  • Emmanuel Nchimbi, ambaye sasa ni balozi wa Tanzania nchini Brazil, amepewa onyo kali, wakati mjumbe mwingine wa Kamati Kuu, Adam Kimbisa amesamehewa.

Dar es Salaam. Licha ya ukweli kwamba wajumbe watatu wa Kamati Kuu ya CCM walitoka nje kujitenga na uamuzi wa chombo hicho, Sophia Simba ndiye anayeangaliwa zaidi baada ya Halmashauri Kuu ya chama hicho kuamua kumvua uanachama tofauti na wenzake.

Emmanuel Nchimbi, ambaye sasa ni balozi wa Tanzania nchini Brazil, amepewa onyo kali, wakati mjumbe mwingine wa Kamati Kuu, Adam Kimbisa amesamehewa.

Simba, mwanasiasa mkongwe aliyekuwa mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) na ambaye amewahi kuongoza wizara mbili tofauti, anaingia kwenye orodha ya vigogo wa juu wa CCM waliowahi kuvuliwa uanachama kwa tuhuma tofauti.

Wengine ni Maalim Seif Sharif, Katibu mkuu wa CUF ambaye alikuwa mwanzilishi wa kikundi cha kupambania demokrasia cha Kamahuru ambacho baadaye kiliunganishwa na chama cha Civic United Front (CUF) ambacho kimejijenga kama chama kikuu cha upinzani visiwani Zanzibar.

 Kada mwingine ni Shaaban Mloo ambaye alifukuzwa CCM mwaka 1988 wakati hali ya kisiasa ilipochafuka Zanzibar. Kama ilivyokuwa kwa Maalim Seif, baadaye Mloo alijiunga na chama kipya cha upinzani kilichoitwa Kamahuru.

Mansoor Yusuf Himid ni kigogo mwingine aliyevuliwa uanachama wa CCM kutokana na misimamo yake. Mansoor, ambaye alikuwa mwakilishi wa Kiembesamaki, pia aliwahi kuwa mweka hazina wa CCM-Zanzibar na Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi wakati wa Serikali ya Dk Amani Karume na Dk Ali Mohamed Shein kabla ya kutimuliwa.