JPM: Katika utawala wangu hakuna atakayepata mimba na kurudi shule

Rais John Magufuli

Muktasari:

  •  Ameyasema hayo leo (Alhamisi) wakati wa ziara yake ya siku tatu mkoani Pwani ambako amezindua viwanda saba.
  • “Azae halafu aende kuwahubiria wenzake, unajua ilikuwa hivi, halafu nilifanya hivi,”amesema.

Pwani. Rais John Magufuli amesema wakati wa utawala wake hakuna mwanafunzi atakayepata mimba na kuruhusiwa kurudi shule.

 Ameyasema hayo leo (Alhamisi) wakati wa ziara yake ya siku tatu mkoani Pwani ambako amezindua viwanda saba.

“Azae halafu aende kuwahubiria wenzake, unajua ilikuwa hivi, halafu nilifanya hivi,”amesema.

Amesema waliozaa shuleni wanaweza kwenda kupata elimu nyingine kama vyuo vya ufundi stadi (Veta) na kilimo badala ya kurudi shule na kuanza kuwafundisha wenzao yale waliyoyafanya.

“Mnataka niwaambie warudi shule halafu, ni bora wakalime ili ile nguvu waliyoitumia kujifungua waitumie kulima,” amesema.

Amesema; “Ni rahisi zaidi kuzalia chuo kikuu, ule mwaka wa kwanza, wa pili lakini sekondari, darasa la kwanza  kupeleka walio na watoto, tunapoteza maadili yetu, watazaa mno.”

 “Mtajikuta darasa la kwanza wote wanawahi nyumbani kwenda kunyonyesha. Hii tutalipeleka Taifa pabaya,” amesema.