Mawaziri tisa watumia jukwaa la JPM ziarani

Muktasari:

  • Mawaziri hao walioongozana na Rais aliyekuwa kwenye ziara ya kikazi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ni pamoja na Profesa Makame Mbarawa (Maji na Umwagiliaji), Ummy Mwalimu (Afya), Isack Kamwelwe (Ujenzi), Luhaga Mpina (Mifugo na Uvuvi), Kangi Lugola (Mambo ya Ndani) na Selemani Jafo (Tamisemi).

Dar es Salaam. Mawaziri sita na manaibu watatu kutoka wizara mbalimbali jana walitumia wastani wa dakika tano kila mmoja kumsaidia Rais John Magufuli kuwaeleza wananchi wa Mkoa wa Singida namna Serikali inavyotekeleza ilani ya CCM kisekta ndani ya mkoa huo.

Mawaziri hao walioongozana na Rais aliyekuwa kwenye ziara ya kikazi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ni pamoja na Profesa Makame Mbarawa (Maji na Umwagiliaji), Ummy Mwalimu (Afya), Isack Kamwelwe (Ujenzi), Luhaga Mpina (Mifugo na Uvuvi), Kangi Lugola (Mambo ya Ndani) na Selemani Jafo (Tamisemi).

Pia, walikuwapo Doto Biteko na Stanslaus Nyongo (manaibu waziri wa Madini) na Naibu Waziri (Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira), Mussa Sima.

Kwa pamoja walitumia jukwaa hilo kuwaeleza ahadi mbalimbali zilizotekelezwa na zinazoendelea kutekelezwa na Rais Magufuli na Serikali yake.

Uzinduzi wa Daraja

Akiweka jiwe la msingi katika ujenzi wa daraja la Mto Sibiti uliopo mpakani mwa Mkoa wa Singida na Simiyu, Rais aliwaagiza watendaji wa idara ya ujenzi na uchukuzi kuhakikisha wanamsimamia mkandarasi anayelijenga ili likamilike mapema.

Alisema kukamilika kwa daraja hilo kutasaidia kuharakisha shughuli za maendeleo katika mikoa hiyo.

Rais alisema Serikali haitawafumbia macho wakandarasi wazembe na alimwagiza Waziri wa Ujenzi, Kamwele kuhakikisha anamsimamia mkandarasi anayelijenga daraja hilo ili likamilike ifikapo Machi, 2019.

“Wananchi hawa waliniamini ndiyo maana wakanipa kura ili niweze kuwaletea maendeleo kupitia rasilimali zao walizonazo, ndiyo maana na mimi sitaki kuwaangusha,” alisema.

Alisema tayari Serikali imemlipa mkandarasi huyo kutoka China ambaye ni kampuni ya Hynan Sh18 bilioni, lakini amekuwa akisingizia maeneo linapojengwa daraja hilo hujaa maji kipindi cha mvua, hali inayokwamisha ujenzi.

Rais Magufuli alipinga utetezi huo na kumtaka afanye kazi usiku na mchana kipindi hiki ambacho mvua zimesimama.

Pia, aliwaagiza watendaji wa Wakala wa Barabara (Tanroads) wahakikishe wanakamilisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami yenye kilomita 24 kwa pande zote za daraja la mto huo.

Waziri wa Ujenzi, Kamwele alimhakikishia Rais kuwa wizara yake imejipanga na itahakikisha inawafuatilia kwa karibu wajenzi wa daraja hilo ili likamilike katika muda uliopangwa.