Meya, madiwani wa Chadema Arusha wakamatwa

Naibu Meya wa Jiji la Arusha, Viola Likindikoki

Muktasari:

  • Meya wa Jiji la Arusha, Kalist Lazaro amesema Viola pamoja na madiwani hao wawili wamekamatwa leo (Alhamisi) wakiwa katika mkutano wa ndani uliokuwa ukisikiliza kero za wananchi.

Arusha. Naibu Meya wa Jiji la Arusha, Viola Likindikoki, pamoja na madiwani wengine wawili wa Chadema wamekamatwa na Jeshi la Polisi mkoani humo kwa sababu ambazo mpaka sasa hazijafahamika.

Meya wa Jiji la Arusha, Kalist Lazaro amesema Viola pamoja na madiwani hao wawili wamekamatwa leo (Alhamisi) wakiwa katika mkutano wa ndani uliokuwa ukisikiliza kero za wananchi.

“Nipo Tanga kikazi na nilimkaimisha nafasi yangu Viola, kwa kawaida Alhamisi tunasikiliza kero za wananchi, wakati wakiendelea kusikiliza kero ndipo walipokamatwa,” amesema.

Wengine waliokamatwa katika tukio hilo ni diwani wa viti maalumu (Chadema), Kata ya Ngarenaro Happiness Charles na diwani wa Viti Maalumu kata ya Olorieni, Sabrina Francis.

Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Charles Mkumbo amesema kwa kifupi kwamba jeshi lake linawashikilia kwa uchunguzi.

Akizungumza na gazeti hili, diwani wa viti maalumu (Chadema), Jenipher Lomayan  amesema madiwani hao wamekamatwa  leo saa 9 alasiri  wakiwa ndani ya ofisi ya Meya wa Jiji la Arusha wakisikiliza kero za wananchi.

Lomayan, amesema  wakiwa ndani ya ofisi hizo polisi waliovalia nguo za kiraia waliingia na kuwaeleza kwamba wako chini ya ulinzi na wanatakiwa kufika mbele ya makao maku ya jeshi hilo kwa uchunguzi zaidi.

“Wale polisi walitaka kuichukua simu ya Naibu Meya na ndipo madiwani wawili (Sabrina na Happiness) wanaoshikiliwa waliingilia kati na kuwazuia polisi wasimnyanganye simu hiyo na ndipo na wao wakaunganishwa katika tukio hilo,” amesema.