Mtanzania Shujaa aibuka kidedea mashindano ya Quran Afrika

Muktasari:

  • Waliohudhuria mashindano hayo ni pamoja na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Dar es Salaam. Mtanzania, Shujaa Suleiman Shujaa ameibuka kidedea katika mashindano ya 19 ya kuhifadhi Quran Afrika na kujinyakulia kitita cha Sh15 milioni.

Shujaa ameibuka mshindi katika kundi la washiriki wa juzuu 30 leo, Mei 27.

Pamoja na mamilioni hayo, Shujaa mwenye miaka 23 ambaye ni mkazi wa Morogoro, amejishindia pia laptop, kiwanja chenye hati eneo la Kigamboni kilichotolewa na kampuni ya Property International ya jijini Dar es Salaam pamoja na dola za Marekani 500 kutoka kwa Ahmed Seif “Magari” aliyetoa dola 500 kwa washindi wote watano.

Akizungumza na maelfu ya waumini na Watanzania waliofurika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam leo mchana Mei 27, 2018 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewataka Watanzania waendelee kuilinda amani iliyopo nchini kwani ikipotea hakuna atakayeweza kufanya ibada.

“Mtakubaliana nami kuwa amani ya nchi yetu, ndiyo inatufanya tutembee vifua mbele dhidi ya wenzetu, ni neema kubwa ambayo kila muumini anapaswa kuilinda kwani ikipotea hata mkusanyiko wetu huu wa leo si rahisi kufanyika mahali kama hapa,” amesema.

 “Leo hii tuko hapa uwanjani kwa sababu tuna amani, kama Serikali isingekuwa inashirikisha Watanzania wote kulinda amani, basi tusingeweza kukutanika hapa. Kuna nchi 18 ziko hapa, na watu wake wamekuja hapa uwanjani kwa kuwa wana uhakika na amani tuliyonayo sisi Watanzania,” alisema.

Mshindi wa pili kwenye kundi hilo la juzuu 30 ni Ahmed Noor wa Sudan ambaye ameshinda Sh12 milioni pamoja na laptop akifuatiwa na Muzamil Awadh Mohamed wa Sudan aliyejishindia Sh7.5 milioni pamoja na laptop zilizotolewa na kampuni ya Camara Education.

Mshindi wa nne ni Abdulally A. Mohammed wa Kenya aliyepata zawadi ya sh. 5,711,000 na wa tano ni Ibrahim Maazur kutoka Niger, aliyepata Sh3milioni.

Washindi hao wote watano walipewa zawadi ya kwenda hijja na Waziri wa Mambo ya Dini wa Saudi Arabia, Dk Saleh Ally Sheikh.