NEC yataka tume huru

Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu, Damian Lubuva .

Muktasari:

  • Mapema mwezi huu, Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu, Damian Lubuva akiwa sambamba na wajumbe wengine wa taasisi hiyo na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), walikabidhi ripoti ya uchaguzi huo kwa Rais John Magufuli.

Dar es Salaam.  Baada ya kukamilisha Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka jana kwa mafanikio, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetoa mapendekezo saba kwa Serikali ili iyashughulikie kwa lengo la kuboresha uchaguzi ujao.

Mapema mwezi huu, Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu, Damian Lubuva akiwa sambamba na wajumbe wengine wa taasisi hiyo na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), walikabidhi ripoti ya uchaguzi huo kwa Rais John Magufuli.

Licha ya kueleza mafanikio yaliyopatikana katika kipindi chote cha mchakato huo, kuanzia uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura, kampeni mpaka upigajikura, NEC imebainisha maeneo yanayohitaji kufanyiwa marekebisho kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2020 au uchaguzi mdogo utakaojitokeza kuwa ni pamoja na Sheria ya NEC.

Tume hiyo imeitaka Serikali kupitia wizara husika, kutunga Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi itakayoiwezesha kutekeleza majukumu yake ya kikatiba kwa ufanisi kama ilivyo kwenye nchi nyingine zilizofanya hivyo.