Polisi waua mtuhumiwa wa ujambazi
Muktasari:
- Kabla ya kufikwa na mauti mtuhumiwa huyo alijeruhiwa miguu na kiuno lakini alifariki akiwa njia kuelekea hospitalini.
Moshi. Mtu anayedaiwa kuwa ni jambazi sugu ameuawa na askari wa jeshi la polisi mkoani Kilimanjaro kwa kupigwa risasi katika majibizano ya risasi kati yake na polisi.
Kamanda wa polisi mkoani hapa, Hamisi Issa amethibitisha kuuawa kwa mtu huyo na kusema kuwa aliuawa Jumapili saa 1.00 jioni katika eneo la Njoro.
Issa amesema mtu huyo alishahukumiwa kufungwa miaka 30 jela mara mbili
mfululizo kwa makosa ya unyang’anyi lakini alikuwa akitoka kwa kukata rufaa na kushinda kesi.
Kamanda Issa amesema baada ya kuawa kwa mtu huyo alikutwa na bastola
aina ya Browing yenye namba CZ83A 514014 na TZCAR96231, ambapouchunguzi wa awali umebaini kuwa bastola hiyo ilipotea baada ya mmiliki wake na aliyekuwa mfanyabiashara maarufu mjini Moshi Joseph Molel(36) kuuawa.
Desemba 10, 2015 mfanyabiashara huyo aliyekuwa na jina maarufu la Tajiri mtoto akiwa nyumbani kwake Msaranga aliuawa na watu ambao hawakufahamika kisha kutokomea na bastola hiyo ambayo imeoneka.
Hata hivyo Kamanda Issa amesema, marehemu huyo aliyefahamika kwa jina la Noel Simbeyi alikuwa na wenzake wawili ambao walikimbia baada ya kushindwa mapigano na kutokomea kusikojulikana.