Chadema yakana kuhusishwa utekaji wa Kibanda

Mwenyekiti wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Freeman Mbowe

Muktasari:

Kauli hiyo aliitoa mjini Shinyanga alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja vya Shycom mjini hapa kuhusu utata wa kukamatwa na kuhojiwa kwa mmoja wa viongozi wa Chadema.

Shinyanga. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema chama chake hakihusiki na mpango wa uchochezi na utekaji unaodaiwa kufanywa na mwanachama wake, Alfred Lwakatare dhidi ya mwandishi wa habari Absalom Kibanda.

Kauli hiyo aliitoa mjini Shinyanga alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja vya Shycom mjini hapa kuhusu utata wa kukamatwa na kuhojiwa kwa mmoja wa viongozi wa Chadema.

“Wanasema eti sisi tumemteka Kibanda, kwa sababu gani, kwa vikosi vipi na kwa silaha zipi, huo mpango wanaujua wao, na tunasema hatutarudi nyuma, wasifikiri kumkamata mpiganaji wetu wataififisha nguvu ya Chadema wanajidanganya” , aisema Mbowe.

Mbowe pia alisisitiza kauli yake ya kuitisha maandamano nchi nzima ya kumshinikiza Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kujiuzulu kutokana na matokeo mabaya ya mtihani wa kidato cha nne mwaka huu kwamba yatafanyika.

Alisema maandamano hayo yamepangwa kuwa siku ya Mei 15, mwaka huu.

Mkutano huo ulitanguliwa na maandamano ya wanachama wa chama hicho na viongozi wao baada ya mkutano mkuu wa Mikoa ya Shinyanga, Simiyu na MaraAwali mbunge wa Jimbo Maswa Mashariki, Sylvester Kasulumbayi aliwataka wakulima wa pamba kutokipigia kura CCM kwa maelezo kwamba kimewaingiza katika dimbwi la umaskini kwa kushindwa kusimamia bei ya zao la pamba.