Watumishi CCM kutafuta mlango wa kutokea

Muktasari:

Rais Magufuli amewaomba wana-CCM kumuombea ili awe na uvumilivu kama wa mtangulizi wake, Jakaya Kikwete katika kukabiliana na utovu wa nidhamu kwenye chama.

Dodoma. Mwenyekiti mpya wa CCM, Rais John Magufuli amezungumzia mambo manne atakayoshughulikia katika chama hicho, hasa kufanya mabadiliko makubwa ili chama kiweze kwenda na wakati.

Pia, Rais Magufuli amewaomba wana-CCM kumuombea ili awe na uvumilivu kama wa mtangulizi wake, Jakaya Kikwete katika kukabiliana na utovu wa nidhamu kwenye chama.

Alisema hayo kwenye hotuba yake ya shukrani baada ya kupata kura zote 2,398, katika uchaguzi uliokuwa wa mgombea mmoja wa nafasi ya mwenyekiti wa CCM uliofanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano wa chama hicho uliopo mjini hapa.

Mwenyekiti huyo mpya alisema utendaji kazi ni suala muhimu, hivyo atajenga chama madhubuti ili kiweze kuisimamia Serikali.