KKKT yasalimu amri, kurejesha Sh129 mil

Muktasari:

Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Arusha, Juventus Baitu alisema taasisi yake inafanya uchunguzi kuhakiki watumishi hewa Hospitali ya Selian inayomikiliwa na kanisa hilo lakini hakutaka kuingia undani wa suala hilo.

Arusha. Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) la Mjini Kati, Dayosisi ya Kaskazini mkoani Arusha, limesema lipo tayari kurudisha Sh129 milioni ambazo zilitolewa na Serikali kwa ajili ya mishahara ya madaktari katika Hospitali ya Selian ambayo linaimiliki.

Hatua hiyo imekuja baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuwahoji baadhi ya watumishi wa kanisa hilo na kuchukua baadhi ya mafaili kwa kile kilichoelezwa kwamba wanachunguza mishahara hewa.

Katibu wa Dayosisi hiyo, Samwel Saiguran alisema juzi ofisini kwake kwamba wapo tayari kurudisha kiwango hicho cha fedha kwa utaratibu, kwani waliwalipa madaktari ambao hawakuwa katika orodha ya watumishi wa Serikali kwa nia njema kuokoa maisha ya Watanzania.

Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Arusha, Juventus Baitu alisema taasisi yake inafanya uchunguzi kuhakiki watumishi hewa Hospitali ya Selian inayomikiliwa na kanisa hilo lakini hakutaka kuingia undani wa suala hilo.