Sikia ya Sekilojo kwa Yanga michuano ya Shirikisho

Muktasari:

Chambua alisema Yanga inacheza soka zuri, lakini inashindwa kutumia nafasi nyingi inazopata uwanjani, hivyo wanatakiwa kufanya maombi ili shetani wa kukosa mabao aondoke.

Dar es Salaam. Nyota wa zamani wa Yanga, Sekilojo Chambua amesema ili timu hiyo ifuzu nusu fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, inatakiwa kwanza kumkemea shetani wa kukosa mabao.

Chambua alisema Yanga inacheza soka zuri, lakini inashindwa kutumia nafasi nyingi inazopata uwanjani, hivyo wanatakiwa kufanya maombi ili shetani wa kukosa mabao aondoke.

Katika mechi tatu ilizocheza Yanga katika hatua ya makundi imefunga bao moja tu, huku safu yao ya ushambuliaji inayoongozwa na Donald Ngoma,  Amissi Tambwe, Simon Msuva iliyofunga mabao 70 katika Ligi Kuu Bara ikiacha maswali mengi juu ya uwezo wao wa kuzifumani nyavu katika mashindano ya kimataifa.