Bingwa wa kubikiri Malawi abainika ana VVU, akamatwa kwa amri ya Rais

Muktasari:

Amri hiyo ya Rais imekuja baada ya kubainika kuwa mwanamume huyo maarufu kwa jina la ‘Fisi’ anaishi na Virusi vya Ukimwi (VVU).

Blantyre, Malawi. Rais wa Malawi, Peter Mutharika juzi alitoa amri ya kukamatwa kwa Eric Aniva ambaye hivi karibuni alibainika kufanya kibarua cha kuwabikiri mabinti wa chini ya umri wa miaka 13 zaidi ya 100.

Amri hiyo ya Rais imekuja baada ya kubainika kuwa mwanamume huyo maarufu kwa jina la ‘Fisi’ anaishi na Virusi vya Ukimwi (VVU).

Mutharika alisema lazima mwanamume huyo akamatwe na hatua kali zichukuliwe dhidi yake kwa kuwa, kwa makusudi alifanya vitendo viovu akijua anaishi na VVU na lengo lake lilikuwa kuwaambukiza mabinti hao.

Aniva aliingia matatani baada ya kukiri katika mahojiano akijinasibu kuwa anaendesha maisha kwa kuwabikiri mabinti na kwamba hulipwa kuanzia dola nne za Marekani mpaka saba ambayo ni wastani wa Sh10,000 kwa kila mtu.

Mwanamume huyo alisema wazazi wa mabinti huwa wanampa kibarua cha kuwavusha kutoka utoto kuingia katika utu uzima na kwamba hatua hiyo ni sawa na tambiko.