Mchungaji aliyenaswa na meno ya tembo kanisani jela miaka 20

Muktasari:

Hukumu hiyo ilivutia hisia za watu wengi wa Manispaa ya Mpanda na mkoa wa Katavi ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda, Chiganga Ntengwa baada ya mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa mahakani hapo na upande wa mashtaka na utetezi.

Sumbawanga. Mchungaji wa Kanisa la Moravian, Wilaya Mlele mkoani Katavi, Godwel Siame amehukumiwa kifungo cha miaka 20 jela baada ya kupatikana na hatia ya kukutwa meno ya tembo yenye thamani ya Sh90 milioni akiwa ameyahifadhi kanisani.

Hukumu hiyo ilivutia hisia za watu wengi wa Manispaa ya Mpanda na mkoa wa Katavi ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda, Chiganga Ntengwa baada ya mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa mahakani hapo na upande wa mashtaka na utetezi.

Katika kesi hiyo upande wa mashtaka uliongozwa na Mwanasheria mfawidhi wa Serikali wa Mkoa wa Katavi, Acheres Mliso na mshitakiwa alitetewa na Wakili Patrick Mwakyusa ambapo upande wa mashtaka ulikuwa na mashahidi sita  na upande wa utetezi ulikuwa na  mashahidi wanne.

 

Awali katika kesi hiyo mwendesha mashtaka wa  Serikali Acheres Mliso alidai kuwa mshiakiwa kosa hilo hapo Mei 5, mwaka huu katika Kijiji cha Usevya Wilaya ya  Mlele.

Ilidaiwa mahakamani kuwa siku ya tukio mshtakiwa ambaye alikuwa ni mchungaji huyo alikamatwa na askari wa hifadhi ya taifa ya Katavi na polisi akiwa na vipande 11 vya meno hayo vyenye uzito wa kilo 20 ndani ya kanisa analoliongoza.

Hakimu Chiganga Ntengwa akisoma hukumu hiyo, alisema kutokana na ushahidi uliotolewa mahakama pasipo shaka imeona mshtakiwa anayo hatia ya kujibu hivyo inampa nafasi ya kujitetea

Katika utetezi wake Mchungaji Siame aliliomba mahakama imwachie huru kwani hakujua kama ndani ya kanisa lake kuna meno hayo na ndiyo maana alipokamatwa hakuwa na mashaka yoyote.

Hivyo mahakama  ilimuhukumu kutumikia kifungo cha miaka 20 jela kuanzia jana na kama hajaridhika na uamuzi huo unaruhusiwa kukata rufaa ndani ya siku  30.