Mtanzania kushiriki mashindano ya upishi Marekani

Chef Oisso kushiriki mashindano ya mapishi Marekani

Muktasari:

Uisso mwenye taaluma ya upishi, atashriki mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika Novemba 8-15, baada ya kufanya vizuri katika upishi wa nyama ‘Best Stake Chef’.

Dar es Salaam. Mtanzania Fred Uisso amechaguliwa kushiriki kwenye fainali za mashindano ya upishi ya kidunia yafahamikayo kama ‘World Food Championships 2016’

Uisso mwenye taaluma ya upishi, atashriki mashindano hayo yanayotarajiwa kufanyika Novemba 8-15, baada ya kufanya vizuri katika upishi wa nyama ‘Best Stake Chef’.
Bodi ya Utalii Tanzania TTB leo imemkabidhi bendera mwakilishi huyo wa Afrika anayetarajia kuondoka nchini Oktoba 28 mwaka huu.
Chef Uisso ambaye ni mpishi mwandamizi katika mgahawa wa Afrikand uliopo Kinondoni, anakuwa Mwafrika wa kwanza kupata nafasi ya kushiriki katika mashindano hayo, ambayo yamefanyika kwa kipindi cha miaka 15 mfululizo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2001 baada ya kufadhiliwa na Red Gold Tanzania.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, Chef Uisso amesema amepata nafasi ya kwenda kushiriki mashindano hayo mwezi ujao Alabama States nchini Marekani baada ya kushiriki kupitia mtandaoni mara kadhaa.

“Walinitambua kupitia kazi zangu ambazo nilizifanya mtandaoni, katika dunia nzima ambao tuliingia katika mtandao huo tulikuwa zaidi ya watu 3700 ambao kila mmoja alionyesha uwezo wake wa kupika vyakula mbalimbali, nilirekodi na kuweka katika mtandao huo na majaji watatuchagua washindi 100 katika kila kipengere,” amesema Chef Uisso ambaye ni balozi wa Red Gold Tanzania.