January aombwa kutatua kero

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira na Muungano), January Makamba

Muktasari:

Mmiliki wa mgahawa wa Golden Shower, John Bennett amedai baadhi ya makanisa yameanza shughuli pasipo kufuata mchakato wa kisheria wa kubadilisha matumizi ya ardhi kwanza.

Moshi. Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira na Muungano), January Makamba ameombwa kushughulikia kero ya makanisa yaliyokiuka sheria ya mipango miji na ile inayozuia uchafuzi wa mazingira, kutokana na kuweka vipaza sauti vya juu na kuendesha shughuli zao hadi usiku.

Mmiliki wa mgahawa wa Golden Shower, John Bennett amedai baadhi ya makanisa yameanza shughuli pasipo kufuata mchakato wa kisheria wa kubadilisha matumizi ya ardhi kwanza.

“Kuna kanisa hapa limeanza mwaka 2003 bila kubadili matumizi ya ardhi kwanza kama sheria ya mipango miji inavyosema hadi mwaka 2013 ndipo wakaomba kubadili matumizi ya ardhi,” amedai na kuongeza kuwa baadhi hutumia vipaza sauti na kuwa kero kwa majirani.

Mkazi mwingine wa mjini hapa, James Selengia amesema kama Waziri Makamba hatafika kutatua kero hizo, watalazimika kumuandikia barua Rais John Magufuli kumuomba aingilie kati suala hilo.