Bodaboda wasio na leseni kukiona

Muktasari:

Mofuga ametoa agizo hilo wakati akizungumza madereva  bodaboda wa Tarafa ya Haydom na kusisitiza kuwa suluhisho la ajali zisizo za lazima kwenye eneo hilo ni leseni na mafunzo ya udereva.

Mbulu. Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Chelestino Mofuga amewataka madereva wa pikipiki maarufu bodaboda wawe na leseni hadi kufikia Januari 31 vinginevyo watachukuliwa hatua.

Mofuga ametoa agizo hilo wakati akizungumza madereva  bodaboda wa Tarafa ya Haydom na kusisitiza kuwa suluhisho la ajali zisizo za lazima kwenye eneo hilo ni leseni na mafunzo ya udereva.

Mofuga amesema ili kupunguza ajali zinazosababisha majeruhi na vifo vya madereva na abiria, hatakubaliana vijana wadogo kuendelea kupata vilema na vifo kutokana na kutokuwa na mafunzo ya udereva.

“Sitakubaliana na mwendelezo wa kupoteza nguvu kazi ya Taifa, hivyo wote hakikisheni mnakuwa na leseni na pindi itakapofika mwishoni mwa Januari nitawaagiza polisi kuwachukulia hatua kali wasiokuwa nazo,” amesema

Pia, amewaagiza madiwani wa kata zote za wilaya hiyo wahakikishe vijana wote wanaoendesha bodaboda wanapatiwa mafunzo na kuwa na leseni za vyombo hivyo.