Mlinzi auawa kwa kupigwa na kitu kichwani

Muktasari:

Mauaji ya mlinzi huyo Kisusi Iddy (40) aliyekuwa akilinda maduka hayo kwenye Mtaa wa Mwatulole, ni muendelezo wa matukio ya kuuawa walinzi wa maduka na mali mbalimbali kwani katika kipindi cha miaka miwili ambacho jumla ya walinzi 20 wameuawa.

Geita. Mlinzi mwingine aliyekuwa akilinda maduka yapatayo 15, mkoani Geita ameuawa kwa kupigwa na kitu chenye ncha kali kichwani.

Mauaji ya mlinzi huyo Kisusi Iddy (40) aliyekuwa akilinda maduka hayo kwenye Mtaa wa Mwatulole, ni muendelezo wa matukio ya kuuawa walinzi wa maduka na mali mbalimbali kwani katika kipindi cha miaka miwili ambacho jumla ya walinzi 20 wameuawa.

Taarifa zilizopatikana jana kuhusu mauaji ya mlinzi huyo na kuthibitishwa na mwenyekiti wa mtaa huo, Fikiri Toi zimeeleza kuwa tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia Januari Mosi na wauaji hao hawakuiba kitu chochote.

Mwili wa Iddy ulikutwa umefunikwa kwa shuka lake alilokuwa akilitumia lindoni, huku likiwa limetapakaa damu.