Mgombea CCM afungwa jela Moshi

Muktasari:

Wakili wa Serikali, Lucy Kiusa amesema mshtakiwa huyo alikutwa na hatia baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, kuridhishwa na ushahidi uliotolewa.

Moshi. Aliyekuwa mgombea udiwani Kata ya Katanini (CCM), Josephat Mushi (45) amehukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela kwa kukutwa na hatia ya kutapeli Sh30 milioni kinyume na sheria.

Wakili wa Serikali, Lucy Kiusa amesema mshtakiwa huyo alikutwa na hatia baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, kuridhishwa na ushahidi uliotolewa.

Hakimu Mfawidhi, Aidan Mwilapwa amesema mshtakiwa ana haki ya kukata rufaa endapo hajaridhika na hukumu hiyo dhidi yake.

Awali, Wakili Kiusa amedai Novemba 4 2015, mshtakiwa alimtapeli Feruli Chua Sh30 milioni kwa kumuuzia kiwanja chake wakati akijua alikichukulia mkopo Benki ya Azania.

Mashahidi wanane kutoka upande wa Jamhuri wakiongozwa na mlalamikaji aliyedai kuwa anafahamiana na mshtakiwa kwa miaka 10 wakiwa wafanyabiashara, amedai alinunua kiwanja hicho bila kujua kama benki iliitoa mkopo.Chua amedai kutokana na uhusiano wake na mshtakiwa alimuamini ndipo alipoamua kuchukua uamuzi wa kununua kiwanja hicho.

Kutokana  na maelezo hayo, Wakili Kiusa alimuuliza swali mshtakiwa kama alishawahi kuwa na kosa kabla.

Hata hivyo, mshtakiwa amedai hakuwahi kushtakiwa.

Wakili huyo, aliiomba Mahakama hiyo kupanga adhabu kulingana na vifungu vya sheria ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Hata hivyo, benki ilipiga mnada kiwanja hicho na kuziba deni ya Sh15.2 milioni iliyokuwa ikidai.