Hukumu ya mama kumuita mtoto mchawi Februari
Muktasari:
Hukumu hiyo itatolewa baada ya pande zote mbili kumaliza kutoa ushahidi wake.
Mbeya. Mahakama ya Wilaya ya Mbeya inatarajia kutoa hukumu Februari 6 ya kesi inayomkabili mwanamuziki wa nyimbo za injili mkoani Mbeya, Aman Mwasote (39) ya kumwita mchawi mtoto wa kike wa miaka tisa.
Hukumu hiyo itatolewa baada ya pande zote mbili kumaliza kutoa ushahidi wake.
Mwasote ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa masomo ya uchungaji katika Chuo cha Biblia cha Southern (SBC) anadaiwa kutenda kosa hilo Septemba 20 mwaka jana saa tisa alasiri katika Viwanja vya Shule ya Msingi Kalobe akiwa kwenye mkutano wa injili.
Mshtakiwa huyo akiwa ameambatana na mashahidi wake wawili, Januari 10, mwaka huu alitoa ushahidi wake akiongozwa na wakili wake, Sambwee Shitambala.
Akijitetea mahakamani hapo, Mwasote alidai Mungu alimuonyesha kuna mtoto ana pepo wa uchawi na kuwaomba wachungaji wenzake waungane kumuombea.
Alidai wakati akimuombea mtoto huyo hakumtaja kuwa ni mchawi.
Akiongozwa na Wakili Shitambala, shahidi Salustian Mkangala alidai anajisikia amani kwa sababu Mungu amenena katika maandiko yake kuwa watafikishwa mbele ya mabaraza kwa ajili ya kazi yake.