Samia awataka CCM kuacha kulialia, watatue kero za watu

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM ambaye pia ni Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan akihutubia wajumbe wa kamati za siasa za matawi mpaka mkoa kwenye kwenye ukumbi wa Sekondari ya Makunduchi Zanzibar juzi. Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais

Muktasari:

Awaeleza kuwa ni muda wa kuwajibika kwa wananchi

Zanzibar. Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi na watendaji wakuu wa chama hicho kuwa wazi kwa kufikisha matatizo yanayowakabili wananchi majimboni kwa viongozi wakuu wa chama hicho ili kupatiwa ufumbuzi haraka iwezekanavyo.

Samia ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Tanzania, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na wajumbe wa kamati za siasa za matawi hadi wilaya huko Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Alisema baadhi ya viongozi na wanachama wamekuwa na utamaduni wa kulalamika wanapokutana na viongozi wakuu, ilhali utatuzi wa kero hizo ni rahisi.

Alisema kwa kuwa viongozi wengi wa CCM ndiyo watendaji wakuu wa Serikali, wakiwamo mawaziri, manaibu mawaziri, makatibu wakuu na wakurugenzi, hivyo ni vyema kuwatumia wakati wowote ili kupata ufumbuzi wa matatizo ya wananchi.

“Huu si wakati wa kuwaogopa viongozi wenu hasa waliomo ndani ya Serikali, kwani kufanya hivyo kunaweza kuleta tofauti kubwa kati ya viongozi na wananchi,” alisema Samia.

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Dk Abdallah Juma Saadalla aliahidi kutumia uwezo na ujasiri wake kusimamia utendaji wa chama hicho.