Dar yanunua gari la kubeba maiti zilizokosa ndugu

Muktasari:

Akizundua gari hilo jana meya wa jiji hilo, Isaya Mwita aliwaambia wanahabari kuwa gari hilo aina ya Isuzu lina thamani ya  Sh 100 milioni.

Dar es Salaam. Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam, imenunua gari la kisasa la kubebea miili ya marehemu waliokosa ndugu na kupeleka katika makaburi kwa ajili ya maziko.

Akizundua gari hilo jana meya wa jiji hilo, Isaya Mwita aliwaambia wanahabari kuwa gari hilo aina ya Isuzu lina thamani ya  Sh 100 milioni.

Mwita ambaye pia ni diwani wa Vijibweni amesema  gari hilo lina uwezo wa kubeba miili minane hadi 16 kwa wakati mmoja.

“Ndani ya gari hili kuna hili mafriji manne na fedha za kununua gari hili zimetokana na mapato ya ndani ya jiji,” alisema Mwita.

“Tumejaribu kuangalia mbadala wa kuhifadhi ndugu zetu wale ambao hawana ndugu, kuna watu wanakutwa katika hospitali zetu hawana ndugu hivyo tumeamua kuleta gari ambalo litasitiri miili yao.

Alisema gari litatumika kwa wakazi wote wa Dar es Salaam na kwamba  gari litakuwa na faida kubwa kwa wananchi wa jiji hilo ambapo awali miili yao ilikuwa ikibebwa na malori.