Upande wa mashtaka kuita mashahidi sita kesi ya Nyerere

Muktasari:

Taarifa ya mashahidi hao kuitwa imetolewa leo Jumanne wakati Nyerere akisomewa maelezo ya awali

Dar es Salaam. Upande wa mashtaka unatarajia kuwaita mashahidi sita na kutoa vielelezo vitatu katika kesi ya kuchapisha maneno yenye nia ya uchochezi kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook inayomkabili mfanyabiashara Yericko Nyerere.

Hayo yalielezwa leo Jumanne na Wakili wa Serikali, Clara Charwe wakati akimsomea maelezo ya awali (PH) mshtakiwa huyo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Respicius Mwijage.

Akisomewa maelezo ya awali, Yericko alikubali maelezo yake binafsi ikiwa ni jina lake, yeye ni mfanyabiashara na kuwa alipelekwa mahakamani na kusomewa mashtaka.

Hata hivyo, aliyakana mashtaka yote yanayomkabili na anatetewa na Wakili Peter Kibatala.

Yericko anadaiwa kuwa Mei 28, 2017 kwa nia ya kuwachochea Watanzania alichapisha maneno kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook.