Uhamiaji kuweka wazi kuhojiwa Askofu Niwemugizi baada ya uchunguzi

Muktasari:

Uhamiaji imeeleza uchunguzi utakapokamilika wataweka wazi sababu za kuhoji uraia wa Askofu wa Jimbo la Ngara - Rulenge, Severine Niwemugizi

Dar es Salaam. Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dk Anna Makakala amesema uchunguzi utakapokamilika wataweka wazi sababu za kuhoji uraia wa Askofu wa Jimbo la Ngara - Rulenge, Severine Niwemugizi.

Dk Anna amesema hayo baada ya kuhojiwa na Mwananchi leo Jumatano kwa njia ya simu kuhusu sababu za kufanya mahojiano kuhusu uraia wa Askofu huyo.

“Hizo ni taarifa za kiuchunguzi, ambazo bado tunaendelea, huwezi ku-disclose kila kitu hata tunayemuhoji hatutakuwa tunamtendea haki, tunapokuwa na doubt ya uraia tunaruhusiwa kuchunguza,” amesema Dk Anna.

Alipoulizwa kuhusu madai ya msimamo wa Askofu Niwemugizi kuhusu Katiba mpya ndiyo pengine umesababisha kuhojiwa uraia wake, Dk Anna amesema hakuna haja ya kueleza chochote kuhusiana na madai hayo hivyo ni vyema kusubiri taarifa za uchunguzi wake.

“Hayo ni yake, sitaki kuongelea hilo, hayo tuyaache,” amesema.