Usajili vitambulisho vya Taifa waanza machimboni Mirerani

Muktasari:

Usajili unafanyika kwenye machimbo eneo la kitalu B (Opec) na kitabu D.


Mirerani. Wachimbaji madini ya Tanzanite katika mji mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro wameanza mchakato wa kupatiwa vitambulisho vya Taifa vitakavyowawezesha kuingia ndani ya machimbo yaliyozungushiwa ukuta.

Ofisa usajili wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) Mkoa wa Manyara, Emmanuel Joshua akizungumza leo Februari 24,2018 amesema baada ya hatua ya kwanza ya usajili kumalizika, kinachofanyika ni kuchukua alama za vidole na kuwapiga picha wachimbaji hao.

Joshua amesema wachimbaji wengi wamejitokeza kujisajili, kazi inayofanyika  kwenye machimbo hayo eneo la kitalu B (Opec) na kitabu D.

Amesema wana wafanyakazi wa kutosha wenye uwezo wa kufanya kazi ipasavyo ili kuhakikisha hakuna vikwazo vinavyojitokeza.

Mmoja kati ya wachimbaji hao, Bakari Baina amesema usajili utakuwa na manufaa kwao kwa kuwa ni haki yao ya msingi kupatiwa vitambulisho vya Taifa.

Baina amesema hata wale wenye kusita kushiriki wanapaswa kujitokeza kwa kuwa mwisho wa siku watashindwa kujulikana wao ni raia wa nchi gani.