Halmashauri ya Jiji Tanga yaibuka kidedea

Muktasari:

Halmashauri nyingine zilizoingia katika tatu bora kwenye mpango huo unaofadhiliwa na UNCDF ni Manispaa ya Ilemela na Jiji la Mwanza

Tanga. Halmashauri ya Jiji la Tanga imeibuka kuwa miongoni mwa washindi watatu kati ya halmashauri nane zilizoingia katika mashindano ya kuibua miradi ya kimkakati ya kuongeza mapato katika bajeti ya mwaka 2018/19.

 

Halmashauri nyingine zilizoingia katika tatu bora kwenye mpango huo unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kukuza Mitaji ya

Maendeleo (UNCDF) ni Manispaa ya Ilemela na Jiji la Mwanza.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Tanga, Daudi Mayeji ametoa taarifa hiyo leo Jumamosi Machi 10, 2018 katika kikao maalumu cha baraza la madiwani  cha kujadili na kupitisha makadirio ya  bajeti ya mwaka wa fedha 2018/19.

 

Amesema miradi ya kimkakati  ipo minne yenye

thamani ya Sh116.9 bilioni.

 

Ameitaja miradi iliyoiwezesha halmashauri hiyo kuingia katika tatu bora kuwa ni ujenzi wa jengo la biashara kituo cha mabasi Kange utakaogharimu Sh8 bilioni, ujenzi wa majengo ya masoko ya

kisasa Mgandini na Makorora yatayogharimu Sh31.6bilioni.

 

Miradi mingine ni ujenzi wa machinjio ya kisasa eneo la Pongwe utakaogharimu Sh8.3bilioni na ujenzi wa jengo la biashara eneo la Tangamano ambao unakadiriwa kutumia Sh68.8bilioni.

 

Kufuatia ushindi huo, wakurugenzi  watendaji wa halmashauri hizo tatu pamoja na waratibu wa miradi,   Machi18, 2018 wanatarajiwa kuwa

miongoni  mwa ujumbe wa watendaji wakuu wa Serikali ya Tanzania watakaokwenda nchini Afrika Kusini kuhudhuria mafunzo ya kuwajengea

uwezo zaidi kuhusu uendeshaji wa miradi hiyo.