Sh400 milioni zatolewa kutoa elimu ya bima

Muktasari:

Wakati wa kusaini mkataba huo wa udhamini Kamishina wa bima nchini Dk Baghayo Saqware amesema kuna changamoto ya wananchi kutotumia huduma za bima kwa wingi na ukuaji mdogo wa sekta hiyo.

 Mfuko wa kuendeleza sekta za kifedha (FSDT) leo umetoa ufadhili wa Sh407 milioni kwa Mamlaka ya usimamizi wa shughuli za bima nchini (Tira) kwa ajili ya utoaji wa elimu ya bima kwa wananchi kama njia ya kutatua changamoto zinazokabili ukuaji wa huduma hiyo.

Wakati wa kusaini mkataba huo wa udhamini Kamishina wa bima nchini Dk Baghayo Saqware amesema kuna changamoto ya wananchi kutotumia huduma za bima kwa wingi na ukuaji mdogo wa sekta hiyo.

 Amesema hali hiyo  husababishwa na uelewa mdogo wa mifumo ya huduma hiyo miongoni mwa watu.

"Sekta ya bima imekuwa kwa asilimia 7 katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, changamoto hii iliyopo ikitatuliwa tutapiga hatua zaidi kwa kuwafikia Watanzania wengi zaidi hususani wenye kipato kidogo na kusisimua mifumo ya usambazaji na utoaji wa huduma za bima," amesema Saqware.