Mbatia aeleza mambo manne ya kujikinga na madhara ya mvua

Mbunge wa Vunjo, James Mbatia akiwasilisha bungeni taarifa binafsi katika kikao cha 36 cha mkutano wa Bunge la Bajeti, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Alikuwa akitoa maeleo binafsi bungeni leo

 


Dodoma. Mbunge wa Vunjo (NCCR-Mageuzi), James Mbatia ametoa mapendekezo manne akitaka yafanyiwe kazi na Serikali ili kuwalinda wananchi na madhara yanayosababishwa na mvua.

Akitoa maelezo binafsi bungeni jana Mei 24,2018 Mbatia amesema mvua zinazonyesha nchini zinaharibu miundombinu na kuwaacha wananchi bila makazi.

Amesema Serikali imeshindwa kutimiza wajibu wake wa kuwakinga, kuwalinda na kuwaokoa  raia wake dhidi ya majanga.

Akiyataja mambo hayo manne amesema, "Kwanza Serikali ijitahidi kulinda uhai huo hasa huduma muhimu za kukuza utu wao mfano huduma za chakula, maji safi na salama, afya, makazi na nyinginezo."

Amesema jambo la pili ni Serikali kuboresha miundombinu ya shule za msingi na sekondari.

“Tatu Serikali irudishe miundombinu ya mawasiliano hususani ya barabara zitakazopitika muda wote,” amesema.

“Jambo la nne ni Serikali kuanzisha wakala wa usimamizi wa majanga kama inavyotakiwa na sheria ili ifanye jukumu moja la kuwakinga, kuwalinda na kuwaokoa raia wake dhidi ya majanga ya aina mbalimbali,” amesema.