Wafanyabiashara wajitolea kuchangishana Sh4 bilioni kujenga nyumba 200 za polisi

Geita. Wafanyabiashara wa Mkoa wa Geita wamejitolea kuchangishana  zaidi ya Sh4 bilioni zitakazotumika katika ujenzi wa nyumba 100 za polisi mkoani humo.

Mradi huo unaotekelezwa katika eneo la makazi ya polisi Mtaa wa Magogo Kata ya Bombambili mjini Geita ukikamilika utapunguza uhaba wa nyumba za kuishi wa askari hao.

Akizungumza leo Ijumaa Mei 25, 2018 wakati wa uzinduzi wa mradi huo jana, mwenyekiti wa kamati ya ujenzi, Chacha Wambura ambaye ni Mkurugeni wa Shule za Waja za mkoani Geita amesema kila mfanyabiashara atajitolea kujenga nyumba kuanzia hatua ya msingi, ukuta na kumalizia kulingana na uwezo wake.

"Kujenga ukuta (boma) hugharimu kati ya Sh15 milioni hadi Sh20 milioni ambapo hadi kukamilika, nyumba  moja itagharimu zaidi ya Sh40 milioni,” amesema.

Amesema kila askari polisi katika mradi huo ataombwa kuchangia kwa hiari angalau mifuko miwili ya saruji.

Huu utakuwa ni mradi wa pili nchini kutekelezwa na wafanyabiashara kwa hiari baada ya ule wa mkoa wa Arusha ambapo wafanyabiashara walihamasishwa na kushiriki ujenzi wa nyumba kwa ajili ya makazi ya askari polisi.