Halotel yapunguza gharama za kutuma fedha

Naibu Mkurugenzi wa huduma za HaloPesa, Vu Tuan Long

Muktasari:

Kupunguzwa kwa gharama hizo kutawawezeha wateja wa mtandao huo kufanya miamala kwa njia ya simu

Dar es Salaam. Kampuni ya Halotel imeondoa gharama za kutuma fedha kwa wateja wake wa Halopesa ili kuwapa unafuu wananchi.

Kutokana na maboresho hayo, wateja wa Halopesa watatuma na kupokea fedha bure ndani ya mtandao huo huku gharama za kwenda mitandao mingine zikipunguzwa pia.

Mkurugenzi wa Halopesa, Vu Tuan Long amesema kuwa kuondolewa kwa gharama hizo kutawawezesha wateja wa mtandao huo walioko vijijini kufanya miamala kwa njia ya simu na hivyo kupunguza gharama za kufanya miamala kwa njia nyingine.

“Tuna mamilioni ya Watanzania ambao kwa mara ya kwanza walipata mawasiliano ya simu tulipoanzisha huduma zetu. Wateja wetu waliopo katika maeneo mbalimbali hasa vijijini wanaweza kutuma pesa bure Halopesa kwenda Halopesa,” alisema Long.

Takwimu za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zinaonyesha asilimia 65 ya Watanzania wote wanapata huduma za fedha huku wengi wakifanya hivyo kupitia simu za mkononi.

Kampuni sita za mawasiliano; Halotel, Vodacom, Tigo, Zantel, Airtel na TTCL ndizo kampuni kubwa za mawasiliano zinazotoa huduma za kifedha kwa njia ya simu.

“Habari njema tuliyonayo kwa wateja wetu ni kuwezeshwa kwa huduma ya Halopesa kutuma pesa kwenda mitandao mingine kwa gharama nafuu zaidi,”