|
Polisi, mahakama zazidi kutajwa kwa rushwa |
Send to a friend |
|
Wednesday, 25 May 2011 21:54 |
|
Minael Msuya IDARA za POLISI na Mahakama zimetajwa tena kuwa ni taasisi sugu zinazoongoza kwa kudai rushwa nchini.Kituo cha Sheria na Haki za binadamu (LHCR) katika taarifa yake imezitaja idara hizo kwamba ndizo kinara kwa kudai rushwa. Hivi karibuni, Taasisi ya Kupambana na kuzuia Rushwa Takukuru) nayo ilizitaja idara hizo kwamba ndizo zilizo mstari wa mbele kudai rushwa nchini.
Ripoti ya mwaka 2010 ya LHCR iliyofanywa katika mikoa 26 nchini na kuhoji watu zaidi ya 5,000, ilibainisha kuwa polisi inaongoza kwa asilimia 65.1 huku Mahakama ikifuatia ikiwa na asilimia 56.4. Akisoma ripoti hiyo, Mwanasheria wa LHCR, Pasience Mlowe alisema polisi na mahakama zinaongoza kwa rushwa na matumizi mabaya ya ofisi na kwamba zinashika nafasi ya 10 kwa Afrika Mashariki.
“Utafiti wa LHCR ulibaini kuwa polisi na mahakama ni taasisi sugu zinazoongoza kwa rushwa na zinashika nafasi ya 10 kwa Afrika Mashariki,” alisema Mlowe.
Alisema Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) nayo inafuatia kwa asilimia 37.8 na kwamba inaendelea kushuka kiwango kila siku ikilinganishwa na 2009 ambapo ilikuwa katika nafasi ya tano. “Hali hii inayonyesha ni jinsi gani baadhi ya watu walivyozitelekeza sheria na haki za binadamu, wananchi wengi wanataabika usiku na mchana, lakini hawapati haki zao stahiki, tunaomba marekebisho ya vifungu vya sheria yafanyiwe kazi ili haki ya binadamu iweze kupatikana,”alisema.
Mlowe alisema, matatizo hayo ya taasisi hizo nyeti za serikali yanachangia kwa kiasi kikubwa kuzorotesha uchumi wa nchi na kwamba serikali inatakiwa kusimamia sheria muhimu. Kwa upande wake ,Mtafiti na Mwanasheria wa LHCR, Onesmo Olengurumwa alieleza kuwa, utafiti huo ulibaini kuwa mauaji ya raia wengi yanasababishwa na vyombo vya dola kutokana na wao kujichukulia sheria mikononi.
“Vifo vya watu 52 vilivyotokea mwaka 2010 vilisababishwa na walinzi wa kampuni mbalimbali na polisi kwa kujichukulia sheria mikononi badala ya kutumia sheria inayowaongoza,”alisema Olengurumwa na kuongeza: ”Mfano mzuri ni wananchi wanaoishi kando ya Mgodi wa North Mara kule Tarime wanauawa bila sababu na ukichunguza utakuta sheria za mgodi, walinzi wa kampuni ndio wanaopaswa kulinda eneo lote sasa serikali inaingiliaje huko,”alisema.
Alisema mauaji ya watu yaliyotokana na mgodi huo, serikali haiwezi kujitetea kwa lolote na kwamba utetezi wake ni wakisiasa. Alisema serikali ikisimamia tume ya sheria na haki za binadamu nchi itaweza kuondokana na changamoto za ukiukwaji wa haki hizo zinazoikabili.
|
Comments