|
Patricia Kimelemeta na Hussein Issa KAMATI ya Bunge ya Nishati na Madini imesema itakutana na Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (Ewura) na Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (Tanesco), kujadili kupanda kwa gharama za umeme huku ikisema itakata rufaa kwenye Baraza la Ushindani Kibiashara kupinga ongezeko hilo.
Mwishoni mwa wiki, Ewura ilitangaza ongezeko la bei ya umeme kwa asilimia 40.29, hatua ambayo imekuwa ikipingwa na wananchi wengi. Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, January Makamba alisema ongezeko hilo limewaumiza vichwa wabunge, jambo ambalo lilisababisha kamati kukaa na kuijadili.
Makamba alisema katika mkutano wake huo na Ewura, kamati hiyo itayapatia mapendekezo yote yaliyowasilishwa na Tanesco pamoja na kukokotoa bei mpya na ile iliyopita ili waweze kujua uhalali wake. “Bei mpya ya umeme imetuchanganya sana, hii inatokana na kuongeza kwa kiasi kikubwa jambo ambalo wananchi wa kawaida watashindwa kuimudu.
Kutokana na hali hiyo, tutakutana na mamlaka husika ili tuweze kujadili na kuangalia hatua zitakazofuata,” alisema Makamba. Kikao hicho ambacho kimepangwa kufanyika juma lijalo, kitajadili bei hiyo na endapo itaonekana haikustahili watakata rufaa.
Alisema Serikali ilitoa Sh200 bilioni kwa ajili ya kununua umeme, ambazo ni sawa na asilimia 60 ya umeme, huku Tanesco ikichangia asilimia 40 akisema kama ingeshindwa kutoa kiasi hicho, gharama za umeme zingekuwa kubwa kuliko zilizotangazwa hivi karibuni.
Viwango vipya Katika ongezeko hilo la bei ya umeme ambalo limeanza kutumika Januari 15 mwaka huu, wateja wa hali ya chini wanaotumia chini ya uniti 50 kwa mwezi, wataendelea kulipa Sh60 kwa uniti wakati watumiaji wa majumbani wanaotumia zaidi ya uniti 50, bei hiyo imepanda kutoka Sh195 hadi Sh273 kwa uniti.
Watumiaji wa kawaida wakiwemo wenye biashara ndogondogo, bei imepanda kutoka Sh157 hadi Sh221 kwa uniti wakati watumiaji umeme mkubwa wa kati, bei imepanda kutoka Sh94 hadi Sh132 kwa uniti, wakati watumiaji umeme mkubwa hasa wenye viwanda na migodi, bei imepanda kutoka Sh84 hadi Sh118 kwa uniti.
Shirika la Umeme Zanzibar (Zeco), litauziwa umeme kwa Sh106 kwa uniti kutoka Sh83 ikiwa ni ongezeko la asilimia 28.21.
|
Comments
Mafuta ya taa bei juu.Gesi ndo haikamatiki,sol a nazo ndo hivyo,Serikali imeamua kutoa adhabu kwa wananchi wake.
Makamba ajue wantania wa leo si wale wa zamani , yeye na serikali lao moja yeye ni sehemu ya kupandishaw bei ya umeme anachotaka ni kutumia pesa za walipa kodi kufanya vikao kuendelea kuwaghiribu wantanzania wakati rufaa yake ni sawa na kuishitaki dowans
Naomba serikali kupitia wabunge iwe na msimamo dhabiti ili kumwokoa mwananchi zaidi ambaye ndiye serikali kwa ujumla.
Ni bora likaongezwa shirika jingine zaid ya TANESCO ilikufanya ushindani zaidi ukwele ni kwamba TANESCO ni shirika mfu.
Umeme ni mtaji wa wakubwa, kama mafuta taa, dizeli na petroli. Nataka mtu mwenye akili timamu anieleze kwa nini Ewura inawapa wenye migodi ruzuku na kuwakamua wananchi. Inaeleweka gharama za uzalishaji kiwandani zikiongezeka, bidhaa kwa mlaji zinapanda automatically. Gharama za migodi zinamaffect vipi mlaji? Hawa ndiyo waliotakiwa kubeba mzigo wote wa ongezeko la bei kwa sababu ni wanyonyaji wakubwa. Wanatuharibia mazingira na kuilipa serikali kiduchu. Sasa walalahoi wanachangia gharama za kuendesha migodi ambayo haina faida kwao. Serikali ya CCM kweli ni KIZIWI!
Tunavyojua sisi mpango wa kuongeza bei ya umeme si katika interest ya kuongeza makusanyo ya shirika, kuna mkono wa wanasiasa walafi na wahujumu uchumi ambao siku zote wamekuwa wakinufaika na TANESCO.