
| TRL yaiingiza Serikali matatani | Send to a friend |
| Tuesday, 24 January 2012 20:42 |
|
MENEJIMENTI ya Kampuni ya Reli nchini (TRL) imeiingiza Serikali matatani baada ya kudai kuwa ndiyo iliyotoa maelekezo kwamba wasisaini makubaliano mapya ya mkataba wa hali bora wa kazi. Madai hayo yalitolewa jana katika Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) wakati wa kusikilizwa kwa kesi iliyofunguliwa na Chama cha Wafanyakazi wa Reli (Trawu), dhidi ya menejimenti hiyo kuhusu mkataba wa hali bora. Katika kesi hiyo TRL inawakilishwa na mwanasheria A. Makundi wakati Trawu inawakilishwa na mwanasheria L. Mwangamba na msuluhishi ni Peter Ngowi Makundi alidai kuwa walipewa maelekezo na Serikali kwamba wasisaini makubaliano mapya ya mkataba wa hali bora wa kazi badala yake wahakikishe wanasaini mkataba ulioisha. Kwa upande wa Trawu, mwanasheria Mwangamba alidai kuwa wanaupinga mkataba huo kwa sababu uko kinyume na sheria ya kazi na kwamba hauwatendei haki wafanyakazi wa TRL hasa pale wanapostaafu. Pia, alidai sheria mpya ya kazi hairuhusu Serikali kuingilia majadiliano yoyote kati ya mwajiri na chama cha wafanyakazi hivyo kwa kutoa maelekezo hayo Serikali imekiuka sheria hiyo. Baada ya kusikiliza hoja zote, msuluhishi aliahirisha kesi hiyo hadi Februari 20 mwaka huu atakapotoa hukumu. Mwishoni mwa mwaka jana wafanyakazi hao kupitia Trawu, walitangaza mgogoro na menejimenti hiyo na kutishia kufanya mgomo endapo matatizo yao hayatatatuliwa. Kesi hiyo ilifunguliwa kupitia hati ya dharura ambapo wafanyakazi wameishtaki menejimenti ya shirika hilo kutokana na kutokuwapo kwa mkataba wa hali bora wa kazi. Majadiliano ya hali bora za kazi yalifanyika Novemba 3 mwaka jana na mkataba ulipaswa kutiwa saini ndani ya wiki moja baada ya kumalizika lakini hadi leo mkataba haujasainiwa. Madai mengine ya wafanyakazi hao ni nyongeza za mishahara kwani kwa mara ya mwisho wanadai nyongeza ziliongezwa mwaka 2008 lakini hadi sasa hakuna kilichoongezeka kwa kupanda daraja au ongezeko la kawaida tofauti na wafanyakazi wenzao wa Rahco ambao wanalipwa vizuri bila kuzalisha. Pia, wanaomba sheria ya Reli ya mwaka 2002 itazamwe upya ili kuondoa urasimu huo uliopo kati ya Rahco na TRL unaozorotesha utendaji wa kazi. Wafanyakazi hao pia wanalalamikia kukosa dhamana kutoka kwa mwajiri wao tangu mwaka 1997 kutokana na Serikali kushindwa kuthibitisha umiliki wa TRL kwa asilimia 100 kimaandishi hali iliyosababisha kushindwa kukopesheka kwenye mabenki. Mwishoni mwa mwaka jana wafanyakazi hao walitangaza mgogoro na menejimenti ya shirika hilo huku wakitaja mambo mbalimbali ambayo walidai yanachangia kurudisha nyuma shirika hilo. Chama hicho kimesema kama hatua yao ya kwenda CMA haitafua dafu basi watatangaza mgomo usiokuwa na kikomo.Baadhi ya madai hayo ni sheria mpya ya manunuzi ambapo waliitahadharisha serikali pamoja na kupita kwa sheria mpya ya manunuzi kutonunua injini za RITE's kwa vile zilikwishathibitika kuwa hazifai na ni chakavu. |















