ACT Wazalendo kutoshiriki uchaguzi Kinondoni, Siha

Muktasari:

  • Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 21, 2018 Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho-Bara, Msafiri Mtemelwa amesema changamoto walizozilalamikia katika uchaguzi wa Januari 13 katika majimbo ya Singida Kaskazini, Songea Mjini na Longido bado hazijafanyiwa kazi.

Chama cha ACT-Wazalendo kimesema hakitashiriki uchaguzi katika majimbo ya Kinondoni na Siha kwa kuwa sababu zilizowafanya wasusie uchaguzi mdogo uliopita,  bado hazijafanyiwa kazi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Januari 21, 2018 Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho-Bara, Msafiri Mtemelwa amesema changamoto walizozilalamikia katika uchaguzi wa Januari 13 katika majimbo ya Singida Kaskazini, Songea Mjini na Longido bado hazijafanyiwa kazi.

Amesema bado chama hicho kitaendelea kushinikiza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kufanya mageuzi katika mchakato wa uchaguzi.

Amesema malalamiko ya chama hicho kwa NEC ni matumizi ya nguvu ya vyombo vya dola dhidi ya vyama vya upinzani kwa lengo la kukisaidia chama tawala CCM.

Uchaguzi wa Siha na Kinondoni unafanyika baada ya waliokuwa wabunge wa majimbo hayo kuhamia CCM Desemba mwaka jana.