Chuo cha Aga Khan chapongezwa

Mkuu wa chuo  cha  Aga Khan Profesa Joe Lugalla 

Muktasari:

  • Pongezi hizo zimetolewa  na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Ardhi, Profesa Eleuther Mwageni wakati wa mahafali ya 13 ya chuo hicho kinachotoa kozi mbalimbali ikiwamo ya ukunga na uuguzi.


Dar es Salaam. Chuo Kikuu cha Aga Khan (AKU), kimepongezwa kwa namna kinavyotoa elimu  inayosaidia kuunga mkono jitihada za Serikali za kuboresha maisha ya raia wake.

Pongezi hizo zimetolewa  na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Ardhi, Profesa Eleuther Mwageni wakati wa mahafali ya 13 ya chuo hicho kinachotoa kozi mbalimbali ikiwamo ya ukunga na uuguzi.

Amesema elimu ni ufunguo wa maisha na kwamba Chuo Kikuu cha Aga Khan wanafanya jambo jema la kusomesha Watanzania na Serikali pekee yake isingeweza.

“Nashukuru sana Aga Khan kwa msaada huu, nyie wenyewe ni mashahidi baadhi ya wahitimu wametoka katika hospitali mbalimbali. Mbali na hili chuo hiki kimekuwa mstari wa mbele kuendeleza tafiti mbalimbali,” amesema Profesa Mwageni.

Profesa Mwageni ambaye aliwahi kuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), alitumia nafasi hiyo kuwaasa wahitimu hao kuwa mabalozi wazuri pindi watakapokuwa wanatekeleza majukumu yao.

"Kumbukeni chochote mtakachokuwa mkikifanya kiwe kizuri au kibaya kitakuwa na  uhusiano na AKU. Nendeni mkasaidie jamii kwa ujuzi mlioupata hapa chuoni," alisema Profesa  Mwageni.

Mkuu wa chuo hicho, Profesa Joe Lugalla amesema chuo hicho ni cha kimataifa na kinawafundisha wanafunzi  kutoka nchi mbalimbali za Afrika Mashariki  zikiwamo za Uganda  na Kenya .

Kwa mujibu wa Profesa Lugalla ambaye  pia ni  Mkurugenzi  Mkuu wa  Taasisi ya Maendeleo  ya Elimu Afrika  Mashariki ya Chuo Kikuu cha Aga Khan (AKU -IED,EA), amesema  jumla wanafunzi 47 waliohitimu, 25 kati yao ni wa ngazi ya shahada ya uuguzi na ukunga na  shahada ya uzamili ya ualimu ni 22.

Mbali na hilo, Profesa Lugalla amesema  suala la elimu na afya  ni muhimu  kwa Taifa linaloendelea ndiyo maana AKU imejikita katika kuiboresha elimu.

"Tunaamini watu wakielimika wana uwezo wa kutambua matatizo yanayowakabili yanayohusiana na maendeleo. Tukiwa watu wenye afya bora ni muhimu  kwa sababu wataweza kutoa mchango wa maendeleo kwenye jamii zao," amesema Profesa  Lugalla.

Mmoja wa wahitimu wa fani ya ukunga na uuguzi, Sofia Sanga amesema amefurahi kuhitimu ingawa haikuwa kazi  rahisi na  inahitaji mtu kujitoa kwa moyo wote na anamshukuru Mungu kuhitimu salama.

"Nitaingia kazini na moyo mwingine nikimpa mgonjwa nafasi ya kwanza kabla ya kitu chochote. Vilevile kwa wale wauguzi wasiotaka kufanya kazi vijijini watambue magonjwa yapo mahali popote haijalishi upo mjini au vijijini wasiangalie masilahi bali wafuate itikadi ya kazi ya ambayo inampa nafasi ya kwanza mgonjwa kabla ya kitu kingine," amesema Sanga.