Ajali ya gari yajeruhi polisi watatu Arusha

Muktasari:

  • Dereva wa gari la polisi amevunjika miguu yote, huenda akahamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.


Arusha. Askari watatu wa Jeshi la Polisi mkoani Arusha wamejeruhiwa vibaya katika ajali iliyohusisha gari la polisi na lori.

Kaimu kamanda wa polisi Mkoa wa Arusha, Yusuph Ilembo amesema kuwa, ajali hiyo imetokea usiku wa kuamkia leo Machi 8 katika barabara ya Tengeru- Arusha saa 9 alfajiri wakati gari la polisi lililokuwa likisindikiza gari la Benki Kuu kupeleka fedha mkoani Tanga lilipogongwa na lori aina ya tipa.

Ajali hiyo iliwajeruhi askari waliokuwa katika gari hilo na dereva kuvunjika miguu yote na kuumia vibaya kichwani. 

Kamanda Ilembo amesema kuwa, ajali hiyo ilisababisha majeraha kwa askari wengine wawili waliokuwa kwenye gari hilo.

Jeshi la polisi linamsaka dereva wa lori ambaye alikimbia baada ya ajali hiyo.