Ajali yaua watatu wakiwa kazini

File Photo

Muktasari:

Ajali hiyo imetokea wakati wataalamu hao wakiwa kazini kusimamia ujenzi wa barabara. Dereva wa gari lililokuwa limewabeba, Juma Nassoro alijeruhiwa na kupelekwa Hospitali ya Wilaya ya Korogwe, Magunga.

Korogwe. Ofisa wa Uhandisi wa Wakala wa Barabara  Tanzania (Tanroad) Mkoa wa Tanga na waendesha mitambo wawili wa kampuni ya ukandarasi, wamefariki dunia papo hapo baada ya gari walilokuwa wamepanda kutumbukia kwenye korongo lenye urefu wa zaidi ya mita 300 katika milima ya Usambara wilayani hapa.

Ajali hiyo imetokea wakati wataalamu hao wakiwa kazini kusimamia ujenzi wa barabara. Dereva wa gari lililokuwa limewabeba, Juma Nassoro alijeruhiwa na kupelekwa Hospitali ya Wilaya ya Korogwe, Magunga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Benedict Wakulyamba amesema ajali hiyo ilitokea juzi saa tano asubuhi katika Kijiji cha Makwei, Kata ya Vugiri, Tarafa ya Bungu.

Wakulyamba amewataja waliokufa kuwa ni Eliapenda Edward (33) ambaye ni Mhandisi wa Tanroad, Noel Madola (22) na Twaha Chande (49) waendesha mitambo wa mkandarasi anayejenga barabara hiyo.