Ajali za Mbeya zilivyowaibua Kangi Lugola na Kamwelwe

Muktasari:

  • Ajali hiyo ilitokea baada ya gari walilokuwa wakisafiria kutoka Tabora kwenda Kambi ya JKT-Itende Kikosi cha 844KJ-Itende kwa mafunzo ya vitendo kupinduka eneo la mteremko wa Mwase-kwa jijini Mbeya barabara ya Mbeya mjini-Chunya.

Juni 14 mwaka huu, watu 13 wakiwamo vijana 10 wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), ofisa mmoja wa JWTZ, dereva na kondakta wake walifariki dunia kwa ajali.

Ajali hiyo ilitokea baada ya gari walilokuwa wakisafiria kutoka Tabora kwenda Kambi ya JKT-Itende Kikosi cha 844KJ-Itende kwa mafunzo ya vitendo kupinduka eneo la mteremko wa Mwase-kwa jijini Mbeya barabara ya Mbeya mjini-Chunya. Ajali nyingine ni ile ya Julai 1 mwa-ka huu, watu 20 walifariki papo hapo na wengine 45 kujeruhiwa baada ya lori kugonga mabasi matatu madogo ya abiria (daladala)’ kwenye mteremko wa Mlima Iwambi-Mbalizi wilayani Mbeya katika barabara ya Tanzania-Zambia.Kufuatia mfululizo wa ajali hizo, Rais John Magufuli aliagiza kuchukua hatua thabiti kuzidhibiti ajali huku akiweka wazi kuwa amechoka kutuma salamu za rambirambi kila siku kutokana na ajali za barabarani wakati hatua hazichukuliwi.“Nishasema nimechoka kutuma salamu za rambirambi. Mfano Mbeya katika wiki mbili yamefululiza matukio mawili haku-na hatua ya kuchukua hata kumwambia RPC (Kamanda wa Polisi Mkoa) au RTO (Kamanda wa Polisi Usalama Barabarani mkoa) ajiuzulu? Wameshakufa watu 40 mnataka wafe wangapi ndio RPC ajiu-zulu? Alihoji Rais Magufuli.Rais Magufuli pia katika salamu zake za rambirambi kwa mkuu wa mkoa wa Mbeya, Amos Makalla kufuatia ajali iliy-oua watu 20 na kujeruhi 45, aliwataka viongozi wa mkoa huo, jeshi la polisi na mamlaka nyingine husika katika udhibiti wa usalama barabarani kujitafakari na kuchukua hatua stahiki kukabiliana na ajali hizo.Inaendelea Uk 26

Baada ya kauli hiyo, kamati ya ulinzi na usalama Mbeya chini ya mkuu wa mkoa huo na kamati ya usalama barabarani Mbeya ilikutana kwa dharura ili kutekeleza agizo hilo kwa vitendo.

Makalla alisema kamati hiyo ilifikia uamuzi wa mambo saba na baadhi yao ni kufufua barabara ya zamani kutoka Iyunga hadi Mbalizi yenye urefu wa kilomita sita ili kuukwepa mteremko wa Iwambi ili magari madogo na ya abiria yapite barabara hiyo.

Maazimio mengine ni kuhakikisha wafanyabiashara wanaofanyia biashara zao ndani ya hifadhi za barabara kuu ya Tanzania-Zambia wanaondolewa haraka.

Vikao vyote vya kamati ya ulinzi na usalama wilaya na mkoa kuweka ajenda ya kudumu ya usalama barabarani ikiwa ni pamoja na kuweka vituo vya ukaguzi wa magari kwenye mteremko wa Iwambi, mlima Nyoka na Mwasekwa (barabara ya Mbeya mjini-Chunya).

Mawaziri watua Mbeya

Wakati Serikali mkoani Mbeya ikiendelea na utekelezaji wa agizo la Rais Magufuli, siku tatu baadaye mawaziri wawili wakiwa katika siku za mwanzo mwanzo za uteuzi wao nao walifika mkoani humo.

Mawaziri hao ni Mhandisi Isack Kamwelwe wa Wizara ya Uchukuzi, Ujenzi na Mawasiliano na Kangi Lugola wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, walitua Mbeya kwa ajili ya utekelezaji zaidi wa pamoja katika kuchukua hatua nyingine kudhibiti ajali.

Waziri Kamwelwe

Akizungumza na wananchi wa Mbalizi baada ya yeye na Lugola kukagua eneo la ajali hiyo, Mhandisi Kamwelwe alimuagiza katibu mkuu wa wizara hiyo kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara mbadala ya kutoka Iyunga hadi Mbalizi ili kuepusha ajali zinazotokea katika mteremko wa mlima Iwambi.

Pia aliiagiza Wakala wa Usimamizi wa Barabara Nchini (Tanroads) kuhakikisha wanasimamia ujenzi huo na ukamilike ndani ya mwezi mmoja kutoka sasa.

“Nimekubali barabara hii ya kilomita sita ijengwe haraka iwezekanavyo kwa kiwango cha lami na ninamuagiza katibu mkuu kutoa fedha. Pia Tanroads hakikisheni ujenzi huu unasimamiwa kwa umakini na ukamilike kwa muda mwafaka,” anasema Mhandisi Kamwelwe.

Anasema barabara hiyo inajengwa kwa dharura lakini Serikali imeshapata fedha kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya ujenzi wa barabara kutoka Igawa wilayani Mbarali hadi Tunduma mkoani Songwe ambayo ndani yake kutakuwa na barabara ya mchepuko kutoka Mlima Nyoka hadi Mbalizi ambayo itatumika kwa magari makubwa ya mizigo.

Mhandisi Kamwelwe anasema suala la ajali limekuwa likiumiza vichwa na katika kuchukua hatua za kukabiliana na ajali hizo wanaendelea kuchukua hatua ikiwamo kuboresha miundombinu ya barabara.

Mbali na hilo, Mhandisi Kamwelwe anasema kwa asilimia kubwa Watanzania wanatumia magari ya mtumba na si mapya hivyo akashauri ufanyike utaratibu wa kuyakagua magari yote yanayonunuliwa yakiwa bandarini kabla hayajaruhusiwa kuingia nchini.

“Na kwa utaratibu wa Serikali tunaotaka kuuchua ni lazima sote tuwe makini, mwenye gari ujue gari lako ni la thamani ya kutembea barabarani?...lakini hata unaponunua itabidi tufike mahala ukitaka kununua gari basi tupeane kibali ili tujue unataka kununua gari gani,” anasema Mhandisi Kamwelwe.

“Na kwa sababu magari yanapitia kwenye bandari zetu itabidi wakati mwingine ukaguzi ufanyike lakini pia ikiwezekana ukaguzi huu ufanyike kila mwezi… hatuwezi kuendelea kupoteza maisha ya Watanzania,” anasema Mhandisi Kamwelwe.

Lugola ampa kibarua IGP

Waziri Lugola amechukua hatua kadhaa ikiwamo kuwawajibisha maofisa wa jeshi la polisi, kulivunja Baraza la Taifa la Usalama Barabarani huku akimpa kibarua ‘kizito’ Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Simon Sirro kutekeleza hatua saba za kimkakati ili kudhibiti ajali za barabarani.

Waliochukuliwa hatua hadi sasa ni aliyekuwa kaimu kamanda wa polisi Mbeya, Mussa Taibu aliyehamishiwa makao makuu ya jeshi hilo jijini Dar es Salaam, na Mbeya kupata kamanda mpya, Ulrich Matei ambaye alikuwa kamanda wa polisi mkoani Morogoro.

Pia Waziri Lugola aliagiza kushushwa cheo hadi kubakiwa na nyota tatu kwa aliyekuwa Kamanda wa Polisi kikosi cha Usalama Barabarani (RTO) Mbeya, Leopald Fungu.

Waziri Lugola pia alimuagiza IGP Sirro kufungia leseni za madereva ambao wameonywa zaidi ya mara tatu huku akisisitiza madereva watakaokamatwa na kufikishwa mahakamani kwa kukiuka sheria za barabarani na kubainika na kosa wafutiwe leseni zao na warudi darasani kusoma upya.

Sambamba na hilo Waziri Lugola pia aliagiza madereva wote wapimwe kiwango cha ulevi kabla ya kuanza safari zote za masafa marefu.

“Kabla askari hajampima dereva kiwango cha ulevi kwenye eneo la mizani, akague logbook, leseni ya dereva na manifest ili kujiridhisha kama anayempima ni dereva halisi wa gari hilo.’

Tatu, Lugola alimtaka IGP Sirro kufanya ukaguzi wa magari, huku akisisitiza mkaguzi wa magari anayekagua mabasi kwenye kituo cha mabasi aandae orodha ya mabasi aliyoyakagua akionyesha majina ya makampuni ya mabasi hayo, namba za usajili wa magari, leseni ya dereva, tarehe ya ukaguzi, muda na mapungufu aliyoyabaini na orodha hiyo iwasilishwe kwa mkuu wa usalama barabarani (RTO) na RPC.

Hatua nyingine ambazo Lugola alizichukua na kumtaka IGP Sirro kushughulika nazo ni kufanya uhakiki wa leseni za madereva, kuhakiki ukaguzi wa magari, kudhibiti mwendo kasi na hatua za kinidhamu dhidi ya maofisa na askari wazembe.

Pia Lugola alimtaka IGP Sirro kuwachukulia hatua za kinidhamu askari wazembe wa mikoa 10 ya kipolisi ambayo imeongoza kwa ajali za vifo na majeruhi katika kipindi cha kuanzia mwaka 2017. Mikoa hiyo ni Ilala, Kinondoni, Temeke, Ruvuma, Mbeya, Shinyanga, Dodoma, Manyara, Tabora na Tarime/Rorya.

Wamiliki wa mabasi

Lugola alitoa wiki moja kuanzia Jumapili kwa kila mmiliki wa basi awe amefunga kidhibiti mwendo katika basi lake huku akibainisha kuwa anazo taarifa kwamba wapo wamiliki ambao hawajafunga vifaa hivyo licha ya kuamriwa kufanya hivyo muda mrefu kwa mujibu wa sheria ya Sumatra.

Alisema baada ya wiki kupita hakuna basi la masafa litakaloanza safari zake bila ya kuwa na kifaa hiki.

“Kwa mabasi ambayo yamefungwa kifaa hicho ninazo taarifa kwamba madereva wasio waaminifu wanavirekebisha kwa ujanja ujanja ambao wanaujua wao ili visiweze kudhibiti mwendo, nasema hivi madereva wa aina hii kamata nyang’anya leseni na wafikishwe mahakamani’.

Kuvunja baraza

Kuhusu kuvunja Baraza la Taifa la Usalama Barabarani na mabaraza yote ngazi ya mikoa kushuka chini, Lugola alisema kwamba katika kikao hicho aliwauliza baadhi ya maswali wajumbe na mwenyekiti wao na kubaini kwamba hakuna baraza linalofanya kazi ya kusimamia utendaji madhubuti unaoweza kudhibiti ajali barabarani.

“Nawauliza wajumbe kila mmoja anionyeshe nakala ya sheria inayowapa majukumu ya kufanyia kazi hakuna hata mjumbe mmoja mwenye nakala hapa. Hii inaonyesha kwamba hatuna baraza ambalo linasimamia mabaraza haya, ambalo linafuatilia utendaji kazi wao na kuona kwamba huko mikoani na wilayani hali ikoje,’’ amesema Lugola.

“Kwa hiyo nimeridhika kwamba tumekuwa tukiendesha mambo lakini hatuna mabaraza yenye wajumbe makini, utendaji makini ambao utadhibiti ajali za barabarani. Sasa kutokana na hali hiyo na kwa dhamana niliyonayo kuanzia sasa ninavunja rasmi baraza hili na kamati zote za usalama barabarani za mikoa na wilaya zote, nitaunda upya,” amesema Lugola.