Aliyeua askari 8 Kibiti auawa na polisi

Muktasari:

Jambazi huyo ameuawa jana saa nane usiku, ndiye aliyehusika uvamizi wa kituo cha polisi Stakishari na katika benki mbalimbali Dar es Salaam

Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limemuua jambazi sugu, Anaf Kapela ammbaye alishiriki katika matukio mbalimbali likiwemo la mauaji ya askari wanane na kupora silaha saba katika tukio la Mkengeni Kibiti mwaka huu.

Kamanda Lazaro Mambosasa amesema matukio aliyoshiriki jambazi huyo ni la mauaji ya Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Newala mwaka 2013, uvamizi wa Kituo cha Polisi Stakishari mwaka 2015, kuua askari watatu na kupora silaha mbili aina ya SMG katika benki ya CRDB eneo la Mbande, benki ya Access iliyopo Mbagala, NMB iliyopo Mkuranga.

Amesema Septemba 12 mwaka huu saa 8 usiku maeneo ya Kivule Chanika walifanikiwa kumuua jambazi huyo ambaye alikuwa kiongozi na mratibu wa matukio yaliyotokea maeneo mbalimbali nchini.

Amesema jeshi la polisi liliweka mtego na kufanikiwa kumkamata mtu huyo baada ya kujeruhiwa kwa risasi wakati akijaribu kukimbia.

Mambosasa amesema jambazi hilo lilifika maeneo ya Kivule kwa ajili ya kuuguza majeraha ya risasi aliyopigwa ambayo alikuwa anatibiwa kwa bibi mmoja aliyekuwa anaishi maeneo hayo baada ya kukimbia operesheni ya Kibiti.

“Askari waliweka mtego muda huo wa saa 8 usiku na kuzingatia nyumba aliyokuwa akipatiwa matibabu lakini badala yake alitokea katika nyumba nyingine alipoona askari alianza kukimbia ndipo akapigwa risasi kwenye goti la kulia, bega chini ya mkono wa kushoto,”amesema