Asakwa kwa kuanzisha kiwanda cha gongo

Muktasari:

Pia, Simeon alisema Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nyang’honge A na mtendaji wake, Bernard Maige (59) wanahojiwa na polisi kwa tuhuma za kula njama na kumtorosha mwanakijiji aliyekutwa na mitambo na zaidi ya lita 300 za pombe ya moshi aina ya gongo.

Kwimba. Mkuu wa Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza, Mtemi Simeon amesema wanamsaka Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Nyang’honge na mwanakijiji anayetuhumiwa kufungua kiwanda cha kupika gongo kijijini hapo.

Pia, Simeon alisema Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nyang’honge A na mtendaji wake, Bernard Maige (59) wanahojiwa na polisi kwa tuhuma za kula njama na kumtorosha mwanakijiji aliyekutwa na mitambo na zaidi ya lita 300 za pombe ya moshi aina ya gongo.

“Tukio hilo lilitokea Februari 14, mwenyewe nilishuhudia uwapo wa kiwanda cha gongo katikati ya makazi ya watu katika Kijiji cha Nyang’honge,” alisema.

Maige alikiri kukamatwa kwa tuhuma za kumpigia simu mtuhumiwa kwa lengo la kumtorosha, huku akiwatupia lawama polisi kuwa wanawalinda watuhumiwa.

Kamanda wa Polisi Mkoani Mwanza, Ahmed Msangi alisema hana taarifa na tukio hilo kwa sababu yupo nje ya mkoa.