Asanteni, wasema watoto wa Lucky Vincent

Muktasari:

Wawili waliongezea maneno mengine ya “Mungu awabariki” na mmoja akazishukuru serikali za Tanzania na Marekani kutokana na kushiriki kufanikisha safari na matibabu yao katika taifa hilo tajiri duniani.


Kilimanjaro/Dar. Neno moja lililosikika kutoka kwa watoto watatu wa Shule ya Msingi ya Lucky Vincent baada ya kuwasili jana ni “asanteni”.

Wawili waliongezea maneno mengine ya “Mungu awabariki” na mmoja akazishukuru serikali za Tanzania na Marekani kutokana na kushiriki kufanikisha safari na matibabu yao katika taifa hilo tajiri duniani.

Watoto hao; Doreen Mshana, Wilson Tarimo na Sadia Awadh, waliwasili jana kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro kwa ndege aina ya DC-8 ya shirika binafsi la American Pulse wakitokea Sioux City katika jimbo la Iowa.

Ilikuwa ni miezi mitatu baada ya watoto hao kuokoka katika ajali ya basi lililotumbukia bondeni Mei 6 na kusababisha wenzao 32, walimu wawili na dereva kufariki papo hapo licha ya jitihada za wasamaria wema kujaribu kuwaokoa.

Jana, kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), wanafunzi wa Lucky Vincent, baadhi ya wakazi wa Arusha, kikundi cha kwaya ya injili, viongozi wa Serikali na watumishi wa umma walikusanyika kuwalaki watoto hao waliokwenda pamoja na madaktari wawili kutoka Hospitali ya Mount Meru na wazazi wao.

Baada ya hotuba za viongozi, watoto hao walipewa nafasi ya kuzungumza na Sadia alikuwa wa kwanza.

“Habari za alasiri. Nataka kushukuru wote kwa kuja. Mungu awabariki,” alisema Sadia akiwa ameshikilia kipaza sauti kwa mikono miwili.

Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu, ambaye aliratibu sehemu ya hafla hiyo, alikuwa akisubiri maneno zaidi kutoka kwa Sadia, lakini akajikuta akirejeshewa kipaza sauti.

Maneno kama hayo alitoa Doreen alipopewa nafasi ya kuzungumza.

“Kwanza nataka kuwashukuru nyinyi wote, pili Mungu awabariki na tatu kuwashukuru wote waliosababisha tufikie hapa,” alisema Doreen, ambaye pamoja na kutembea akiwa anasaidiwa wakati akishuka kutoka katika ndege hiyo, alizungumza maneno hayo akiwa amekaa kwenye kiti cha magurudumu.

Wilson aliamua kushukuru serikali zote mbili kwa kufanikisha matibabu yao.

“Naishukuru serikali ya Marekani na Tanzania. Asante sana,” alisema Wilson ambaye anaonekana kuwa nafuu zaidi ya wengine.

Doreen, ambaye alivunjika sehemu kadhaa na ambaye alikuwa anakaribia kupooza kama si jitihada za madaktari, alitoka katika ndege hiyo akitembea bila ya msaada ya magongo na baadaye wahudumu wakaenda pembeni yake kumsaidia kushuka ngazi, huku umati uliokusanyika uwanjani hapo ukipiga makofi.

Aliondoka akiwa hawezi kuzungumza kutokana na kuvunjika taya, lakini jana alikuwa akizungumza ingawa kwa shida kiasi.

Watoto hao, ambao kwa pamoja walivunjika mifupa mara 17 katika ajali hiyo, walipelekwa Hospitali ya Mount Meru baada ya kuokolewa na wakazi na watu wengine, wakiwemo madaktari watatu wa Taasisi ya Elimu ya Afya ya Siouxland na Tanzania (Stemm), ambao walifanya jitihada za kutafuta msaada wa matibabu Marekani.

Akizungumza uwanjani hapo, mbunge wa Bunge la Marekani, Steve King alieleza jinsi alivyotumia dakika tatu kuwasiliana na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, Ikulu ya Marekani, na rais wa Stemm, Dk Steve Meyer kufanikisha safari na matibabu ya watoto hao.

King, ambaye aliwaelezea watoto hao kwa jina la “Watoto wa Muujiza”, alisema alipata simu hiyo wakati akiwa katika shughuli zake nchini Bosnia-Hersegovina na kuwasiliana na wenzake katika muda huo mfupi.

Naye Dk Meyer, ambaye aliongoza matibabu ya wanafunzi hao, alisema uwanjani hapo kuwa yalikuwa ni magumu hasa kutokana na kuwa na majeraha makubwa mwilini lakini wamejitahidi kuwapatia matibabu yote ya msingi.

Alisema haikuwa kazi rahisi kuhakikisha wanawapatia tiba wanafunzi hao kwani majeraha mengine haikuwa rahisi kuonekana bila vipimo, lakini alimshukuru Mungu kwa kuwezesha wote kupata matibabu ambayo yamewasaidia.

“Jopo la madaktari ambalo lilikuwa linatoa huduma, lilifanya kazi kubwa kuokoa maisha ya watoto hawa tunashukuru wameondoka Marekani wakiwa wamepata matibabu yote ya msingi,”alisema

Dk Meyer ambaye alikuwepo siku wanafunzi hao wakipata ajali, akiwa katika shughuli za utalii hapa nchini alisema licha ya kupatiwa matibabu, pia waliweza kupata mazoezi ya viungo ambavyo pia yamesaidia sana kuwafanya wapate nafuu haraka zaidi.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Samaritan Purse, Ed Moore alisema wanashukuru watoto hao wamepata matibabu na wamerejea Tanzania salama.

Alisema licha ya kusaidia matibabu pia wamekusanya vifaa tiba mbalimbali zaidi ya tani 35 ambazo watagawanywa katika hospitali nchini ili kusaidia kuboresha huduma za afya.

“Tunashukuru Serikali ya Tanzania kwa kukubali kupokea msaada huu, ambao tunaamini utasaidia sana kuboresha huduma za afya”alisema.

Nyalandu awapa furaha manusura

Mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu ambaye ndiye aliwezesha safari za watoto hao kwenda Marekani na kurudi alisema taasisi ya Stemm itagharamia masomo ya watoto hao hadi chuo kikuu. “Taasisi hii ya Stemm itagharamia masomo ya watoto hawa popote watakapotaka duniani,” alisema Nyalandu ambaye ni mwenyekiti mwenza wa taasisi hiyo.

Nyalandu alimshukuru Mungu kuwavusha watoto hao katika mitihani migumu iliyowakabili na hatimaye kuwarudisha nyumbani wakiwa wazima wa afya.

Aliwashukuru wafadhili wote kwa kitendo hicho kikubwa cha kuokoa maisha ya watoto hao na pia kusaidia hospitali hapa nchini kwa kutoa vifaa mbalimbali kutoka Marekani ambavyo vitasaidia kuinua huduma za afya hapa nchini.

Wazazi wa watoto hao walioenda na watoto hao kwenye matibabu walikuwa na shukrani pia.

Mzazi wa Wilson, Neema Matemba alisema anashukuru wafadhili hao waliowasaidia watoto hao na kuweza kurudia hali zao za kawaida.

Neema alisema huduma za Marekani ni nzuri na wana utaalamu wa kutosha pamoja na vifaa vya kisasa ambavyo vimefanikisha kupona kwa watoto hao.