Ashikiliwa akituhumiwa kujeruhi kwa msumeno

Muktasari:

Wafanyakazi watano katika ofisi hiyo ya bima ya afya walijeruhiwa, mmoja akielezwa kuwa na hali mbaya.

Geneva, Uswisi. Polisi nchini Uswisi imesema inamshikilia mtuhumiwa anayeaminika kufanya shambulio na kujeruhi watu kwa kutumia msumeno Jumatatu, Julai 24.

Taarifa zinasema shambulio hilo lilifanyika ndani ya ofisi ya umma inayoshughulika na masuala ya bima.

Polisi imesema mtuhumiwa huyo mwenye umri wa miaka 51, amekamatwa kilomita 60 nje ya mji wa Schaffhausen, ambako shambulio hilo lilifanyika.

Imeelezwa kuwa wafanyakazi watano katika ofisi hiyo ya bima ya afya walijeruhiwa, mmoja akielezwa kuwa na hali mbaya.

Habari zinasema kabla ya kutekeleza tukio hilo, mtuhumiwa alikuwa akifuatiliwa na polisi.