Askari afariki dunia akisubiri mafao kambini

Muktasari:

Askari huyo alistaafu Julai 2014 lakini hadi anapatwa na mauti hayo Agosti Mosi mwaka huu alikuwa akiishi katika kambi ya polisi mjini Nansio.

Ukerewe. Askari polisi mstaafu wa kituo cha polisi Nansio wilayani Ukerewe, mkoani Mwanza Msafiri Bundala (52) amefariki dunia kambini kwake akisubiri stahiki zake tangu alipostaafu miaka miwili iliyopita.

Askari huyo alistaafu Julai 2014 lakini hadi anapatwa na mauti hayo Agosti Mosi mwaka huu alikuwa akiishi katika kambi ya polisi mjini Nansio.

Mjane wa marehemu, Paulina Ramadhan (43) aliyeachiwa watoto wanne alisema mumewe aliishiwa nguvu ghafla wakati anarejea nyumbani juzi usiku na alikufa muda mfupi baada ya kufikishwa hospitali.

Alisema mipango ya kusafirisha mwili wa marehemu kwenda Kijiji cha Muhogolo, Kahama mkoani Shinyanga kwa mazishi imekamilika.

Alisema fedha za kusafirishia mwili wa marehemu zimechangwa na askari, ndugu jamaa na marafiki na zitatumika.

Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Dk Titus Kaniki alisema Bundala alifikishwa hospitali akiwa tayari amefariki dunia.