Baba adaiwa kumpa mimba binti yake

Muktasari:

Mjanja (48) mbali na kumpa mimba mtoto wake huyo wa pili, anadaiwa kufanya naye ngono kwa miezi tisa, wakiishi pamoja kama mume na mke.

Dodoma. Mkazi wa Bahi mkoani Dodoma, Omari Mjanja anatuhumiwa kumpa mimba binti yake (jina limehifadhiwa) mwenye umri wa miaka 18 huku shemeji yake akichukua mahari ya mbuzi wawili kuhalalisha jambo hilo.

Tukio hilo limetokea katika Kitongoji cha Chiwela, Kijiji cha Ilindi ambako Mjanja anaishi na binti huyo nyumba moja baada ya kufiwa na wake zake wawili, akiwamo mama mzazi wa binti huyo.

Mjanja (48) mbali na kumpa mimba mtoto wake huyo wa pili, anadaiwa kufanya naye ngono kwa miezi tisa, wakiishi pamoja kama mume na mke.

Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Mjanja alikiri kulala na binti yake mara moja na kwamba wakati huo alikuwa amelewa na alipoamka alijikuta chumbani kwa binti huyo. Alikana kuwa mimba aliyonayo binti huyo ni yake.

“Nilikwenda kulala naye siku moja tu, napo nilikuwa nimelewa sana, lakini mimba naona siyo yangu maana alikuwa anatembea na kijana mwingine hapa ambaye tulimuuliza akakataa, sasa hadi wakapime hospitalini wajue kama ni mimba yangu au ya huyo kijana,” alisema Omari.

Binti huyo alisema tangu msimu wa kilimo ulipoanza (Januari), baba yake alianza kuingia chumbani kwake na kuanza kufanya naye tendo la ngono huku akimzuia kusema kwa watu wengine.