Babu Seya, Papii Kocha mambo safi

Muktasari:

Wasanii hao wamepanga kuja kivingine Februari, 2018 

Dar es Salaam. Wanamuziki Nguza Viking maarufu ‘Babu Seya’ na mwanae Johnson Nguza ‘Papii Kocha’ wamesema Februari, 2018 nyimbo zao zitaanza kusikika maeneo mbalimbali nchini.

Kauli hiyo imetolewa jana Februari 9, 2018 na Papii Kocha wakati akizungumza katika kipindi cha Shilawadu kinachorushwa na televisheni ya Clouds, huku akiwataka Watanzania kukaa mkao wa kula kuwapokea upya.

Babu Seya, ambaye ni mtunzi wa kibao maarufu cha “Seya”, na mwanaye Papii Kocha wameshirikiana katika wimbo huo, ni miongoni mwa wafungwa 8,157 waliosamehewa na Rais John Magufuli siku ya Uhuru wa Tanganyika.

Walikuwa kati ya wafungwa 61 waliokuwa na adhabu za vifungo vya maisha na kunyongwa ambayo si rahisi kupata msamaha wa kawaida wa mkuu wa nchi unaotolewa siku ya sherehe hizo.

Baada ya msamaha huo, familia ya wanamuziki hao ilikwenda Ikulu kumshukuru Rais John Magufuli na siku chache baadaye Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Juliana Shonza aliwakutanisha na uongozi wa studio ya Wanene iliyokubali kuchukua jukumu la kuwarejesha tena katika muziki.

Watangazaji wa Clouds walizungumza na wanamuziki hao nje ya studio za Wanene ambako walikuwa wakiendelea na taratibu za kuandaa nyimbo zao.

“Wakati wowote tutatoa nyimbo na mwezi huu (Februari) Watanzania wakae mkao wa kula. Tunajua Watanzania wanatupenda na sisi tunawapenda. Matatizo tuliyopata ni makubwa kwa sasa tunahitaji sapoti yao tuweze kula, hata ngozi irudi vizuri tupake mafuta mazuri,” amesema Papii Kocha.

Alipoulizwa tukio ambalo hatalisahau, amesema ni ndugu zake waliofariki dunia wakati akiwa amefungwa.

Kuhusu mahusiano ya kimapenzi baada ya kutoka jela amesema, “Miaka 14 nayo ni mingi maisha yanatakiwa yaendelee. Hata mheshimiwa aliniambia nioe.”

Watangazji wa kipindi hicho walipomuuliza kama tayari amepata mchumba, Papii Kocha amesema, “Sijampata ila natafuta bwana si unajua lazima uangalie kwanza. Hata Diamond ameimba wimbo kwamba wazuri ni wengi ila kumpata mwenye mapenzi ya kweli ndio balaa. Michepuko haina dili.”

Papii Kocha alipoulizwa ni kitu gani kiliwakuta mpaka wakahukumiwa kifungo cha maisha amesema, “Unajua Mussa alipochapa fimbo bahari ya shamu aliagizwa na Mwenyezi Mungu akawatoe watu wake awapeleke kwenye nchi ya ahadi. Ya Misri tuachane nayo tuangalie ya Kaanani.”

Kwa upande wake Babu Seya alipoulizwa tukio ambalo hatolisahau katika maisha yake amesema, “Tukio baya ni kufungwa kwa miaka hiyo yote na tukio la pili ni ule waraka tuliomuandikia Rais ambao Shilawadu mliusoma. Tunawashukuru sana.”